Na Salma Said
BODI ya Mapato ya Zanzibar imeamua kuwatambua rasmi wafanyabishara wanaotembeza bidhaa mikononi maarufu kwa jina la Machinga na imetangaza kuwapatia beji maalumu, ili wapate kulipa kodi kwa lengo la kuongeza mapato ya serikali.
Meneja wa Elimu kwa Walipa Kodi, Rashid Ali Juma, alitoa kauli hiyo wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa Habari katika ofisi za Bodi hiyo, iliyopo Kilimani, visiwani hapa juzi.
Alisema, lengo kuu la mpango huo ni kuwaisaidia wafanyabishara hao kutambulika na serikali. Tena Bodi hiyo inatambua kuwa, mchango wa machinga unaweza kuongeza pato la taifa tofauti na sasa ambapo vijana hawa hufanya kazi zao bila kulipa kodi.
Meneja huyo aliongeza kuwa, wafanyabishara hao wamekuwa wakikwepa kulipa kodi kutokana na kutotambulika na serikali, hivyo mpango huo utasaidia kuongeza pato la serikali kwa ajili ya maendeleo ya nchi.
“Mapato kutoka kwa wafanyabiashara wadogo wadogo hayapatikani kwa sababu sekta hiyo hatujaitambuwa rasmi. Tutawapa beji maalumu za kufanya biashara zao huku wakilipa kodi serikalini,” alisema.
Juma alifafanua kuwa, wafanyabishara hao wamekuwa wakiingiza mapato makubwa mifukoni mwao kutokana na biashara wanazofanya kila siku, lakini serikali haipati kitu kutoka kwao.
Alisema ni kweli wafanyabishara hao ni muhimu katika nchi na wanahitajika sana, lakini ni vema kuwawekea utaratibu maalumu wa kulipa kodi kwani nchi yoyote inajiendesha kutokana na kodi za wananchi.
Mchinga visiwani hapa kwa sasa wameongezeka maradufu sababu kubwa ikielezwa kutokana na wengi wao kufukuzwa jijini Dar es Salaam na kisha kukimbilia visiwani hapa.
“Tatizo kwa wafanyabiashara hawa hawana sehemu za kufanyia biashara zao, kwa maana hiyo hawakubaliki kihalali na ndio maana wanapata usumbufu wa kuhamishwahamishwa,” alisema
Alisema, mpango huu upo katika mkakati wa miaka mitano kufanywa na Bodi ya Mapato ya Zanzibar (ZRB), ambapo kuna lengo la kukusanya mapato katika maeneo yote muhimu.
Bodi ya mapato imekusudia kukusanya kodi jumla ya Sh. Billioni 60 kwa mwaka wa fedha 2006/2007, ambapo mianya yote iliyokuwa ikivujisha mapato na kulikosesha taifa fedha inatarajiwa kuzibwa.