Na Oswald Rutaihwa
WAKATI Watanzania bado wanahoji sababu za serikali kuwekeza mabilioni ya shilingi katika ujenzi wa maghorofa pacha ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) yanayojulikana kama minara pacha, kumeibuka kashfa ya unyanyasaji na udhalilishaji wa wazawa wanaofanya kazi katika mradi huo.
Ushahidi ambao umekusanywa kwa wiki kadhaa sasa, unaonyesha kuwa wafanyakazi wazawa wamekuwa wakifananishwa na nyani na kutukanwa matusi ya nguoni na baadhi ya vigogo wa kampuni ya Group Five ya Afrika ya Kusini ambayo ilishinda zabuni ya ujenzi wa majengo hayo yenye thamani zaidi ya Sh280 bilioni.
Katika moja ya matukio ya hivi karibuni, Ruan Kidson, raia wa Afrika Kusini ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha Ulinzi na Usalama katika kampuni ya Group Five anadaiwa kumdhalilisha Pius Masekesa, Mtanzania aliyeajiriwa kama fundi makanika kwa kumfananisha na sokwe mweusi.
Kidson ambaye ni Mzungu, mbali ya kumfananisha Masekesa na sokwe, pia anadaiwa kumtisha kwa kumuonyesha mlalamikaji picha za watu wanaoteswa alizozihifadhi kwenye kompyuta yake.
Tayari, Masekesa amejaza fomu ya malalamiko kwa uongozi wa Group Five kuelezea vitendo hivyo na kutaka hatua za kinidhamu zichukuliwe dhidi ya mzungu huyo.
Kwa mujibu wa ushahidi tulionao, uongozi wa Group Five umeamua kuitisha kikao cha nidhamu kitakachowahusisha pia viongozi wa tawi la wafanyakazi ili kumaliza tatizo hilo.
"Huyu ofisa (Ruan Kidson) ataitwa kwenye kikao cha kamati ya nidhamu kitakacho wahusisha viongozi wa chama cha wafanyazi ili kutatua tatizo hili kwa sababu limekuwa likijirudia," inasema sehemu ya fomu ya malalamiko iliyojazwa na uongozi wa kampuni hiyo.
Habari za kunyanyaswa kwa wazalendo katika mradi wa ujenzi wa minara pacha zimeibuka huku Watanzania wakiwa hawajaelezwa sababu za msingi za serikali kutumia mabilioni ya fedha katika mradi huo.
Vitendo vya unyanyasaji kwa wafanyakazi wazawa katika maeneo mbalimbali nchini vimekuwa vikiongezeka na tukio la hivi karibuni kabisa likiwa ni la kupigwa na kuumizwa kwa mfanyakazi katika maeneo ya kazi.
Pia, kama hilo halitoshi katika maeneo ya migodini katika sehemu mbalimbali nchini, wafanyakazi wazawa wamekuwa wakifyatulia risasi wakazi wa maeneo hayo na hivyo kuleta madhara.
Mwenyekiti wa wa Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC), John Cheyo, mwaka jana alihoji bungeni matumizi makubwa ya fedha yanayofanywa na uongozi wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) bila Bunge kuwa na taarifa yoyote.
Akichangia katika muswada wa sheria ya BoT uliowasilishwa bungeni na Waziri wa Fedha, Zakia Meghji, Cheyo alionyesha kushtushwa na taarifa za benki hiyo kutumia mabilioni ya fedha kujenga majengo yake mapya bila Bunge kuwa na taarifa.
Hadi sasa inadaiwa kuwa zaidi ya sh280 zimekwisha kutumika katika ujenzi wa majengo hayo