WAJUMBE wa Kamati za Maendeleo ya Kata (WDC), wilayani Kahama, wamegoma kuhudhuria vikao vya kuwajadili wakopaji wa sh bilioni moja iliyotolewa na Rais Kikwete hadi watakapolipwa posho za vikao hivyo.
Habari zilizopatikana kutoka ndani ya Tawi la Benki ya NMB, Kahama na kuthibitishwa na Meneja wa tawi hilo, Leon Ngowi, zilisema vikao vya kuwathibitisha waombaji kutoka katika kata vimekwamisha utoaji wa Fedha hizo.
Ngowi, alisema fomu za waombaji zimejazana katika benki hiyo lakini mihutasari na barua za kuwathibitisha waombaji hazijawasilishwa kutoka kwenye kata, kutokana na taratibu zilizowekwa na benki hiyo kushindwa kutoa pesa hizo.
Alisema pamoja na kuwa pesa hizo zipo tayari lakini benki hiyo inasubiri vikao vya WDC ili kupata uthibitisho wa walioomba na maeneo yao ya biashara kutambuliwa na wajumbe wa kamati hiyo.
Baadhi ya wajumbe wa kamati za maendeleo za kata ambao hawakupenda kutaja majina yao walisema hawezi kukaa hadi watakapolipwa posho za vikao vya kujadili maombi hayo ya wajasiriamali wanaotaka kuchukua hiyo bilioni ya Kikwete.
Aidha, kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Kahama, Ofisa Ushirika Marco Nzingura, alisema pesa hizo za mikopo haziwezi kutumika kuwalipa posho wajumbe.
Awali Tanzania Daima ilibaini kuwa fomu za kuomba mkopo huo zinauzwa kati ya sh 2,000 hadi sh 5,000 kwa wale wanaozitafuta.
Aidha, waombaji hao wamelalamikia kukatwa kati ya sh 5,000 hadi sh 20,000 kwa ajili ya mchango wa sekondari za kata.