MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Rukwa, imemhumuku Mtoto, Spriano Done (14), mkazi wa Jangwani kuchapwa viboko viwili kwa kosa la kumbaka mtoto mwenzie mwenye umri wa miaka minne.
Hukumu hiyo imetolewa jana na Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo, Luzango Khamsini, baada ya kuridhika na ushahidi uliotolewa na upande wa mashitaka.
Ilidaiwa mahakamani hapo na Mwendesha Mashitaka wa Polisi, Cleophace Mginge kuwa mshitakiwa Spriano alitenda kosa hilo Oktoba 29, 2006.
Mginge aliiambia mahakama kuwa mshitakiwa alitenda kosa hilo baada ya kukutana na mtoto huyo wakati akitoka shule.
Mahakama ilielezwa kuwa Done yupo chini ya umri wa miaka 18, na ni mara yake ya kwanza kutenda kosa hilo, na mara yake ya kwanza kufikishwa katika mahakama.
Katika utetezi wake alioutoa mahakamani hapo, Done aliiomba mahakama kumpunguzia adhabu kwa kuwa ni mtoto na wakati anatenda kosa hilo hakujua jambo alilokuwa akilifanya.
Upande wa mashitaka ulikuwa na mashahidi watatu na upande wa mshitakiwa ulileta mashahidi wa utetezi wawili.
Hata hivyo, Hakimu Khamsini alitoa adhabu ya kuchapwa viboko viwili kwa mtoto huyo na kumuachia huru kwa sharti la kutorudia kutenda kosa hilo tena.
Hivi karibuni, huko mkoani Tabora, mtoto wa mika 15 alihukumiwa kifungo cha miaka 15 kwa kosa la kumbaka mtoto wa miaka mitatu.