Na Mwandishi Wetu, Mbeya
MAHAKAMA Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya, imeanza kusikiliza rufaa mbili zilizotolewa na pande mbili katika kesi ya dawa za kulevya inayowakabili watu 13 wanaodaiwa kusafirisha cocane kwa kutumia mwili wa marehemu Kombo Siriri.
Kufikishwa kwa watuhumiwa hao mbele ya mahakama hiyo kunatokana na rufaa mbili zilizokatwa na mawakili,upande wa Jamhuri ukipinga uamuzi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya kujitoa kusikiliza kesi hiyo na upande wa utetezi kupinga kunyimwa dhamana.
Jaji Simon Lukelelwa alimtaka Mwendesha Mashitaka, Ayub Mwenda, uliokata rufaa namba 15 ya mwaka 2007 kupinga uamuzi wa mahakama ya Hakimu Mkazi Mbeya kujiondoa kuisikiliza kwa madai kuwa haina mamlaka nayo.
Jaji alisema hoja za rufaa hiyo na ile ya upande wa utetezi namba 9 pia ya mwaka huu, zinapaswa kuwasilishwa kwa maandishi kwenye mahakama hiyo ili apate kuyapitia kwa umakini zaidi kabla ya kuamua rufaa hizo.
Jaji huyo alisema kwa kuwa rufaa zote mbili zinapinga suala moja, ni vyema zikaunganishwa na kuwa moja ili maamuzi yatakayotolewa yalingane na kuokoa muda kuliko kila rufaa ikasikilizwa kwa wakati wake.
Wakili Mwenda aliiahidi Mahakama Kuu kuwa ifikapo Machi 14, hoja za upande wa Jamhuri zitakuwa tayari kimaandishi pia upande wa utetezi ukiongozwa na Wakili Mike Mbise, uliomba kuwasilisha hoja zao kwa maandishi Machi 12.
Jaji Lukelelwa alikubaliana na upande wa utetezi na kuutaka uwasilishe rufaa hiyo kwa maandishi kama walivyoomba na akaongeza kuwa Mahakama Kuu itatoa uamuzi wa rufaa hizo Machi 20 mwaka huu baada ya kupitia hoja za maandishi.
Baada ya mahakama kuu kuzipokea rufaa hizo na kutaka
ziandaliwe kimaandishi, watuhumiwa wote 13 walirudishwa rumande hadi Machi 20 mwaka huu hadi rufaa hizo zitakapotolewa maamuzi.
Watuhumiwa hao 13 walikamatwa Desemba 13 mwaka jana, wakikabiliwa na makosa manne ambayo ni kula njama, kuingiza, kusafirisha na kukutwa na dawa za kulevya aina ya cocane zenye thamani ya Sh23.8 milioni.