NDOTO za aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Ukiwana Ditopile Mzuzuri, kupata dhamana na kurudi uraiani, ziliyeyuka jana katika viwanja vya Mahakama Kuu baada ya mahakama hiyo kushindwa kusikiliza maombi yake ya dhamana katika kesi ya mauaji inayomkabili.
Mahakama hiyo ilishindwa kusikiliza ombi hilo kutokana na kile kilichoelezwa kuwa ni mawasiliano mabovu kati ya Polisi na Magereza.
Jaji Augustine Mwarija, aliyepangiwa kusikiliza ombi hilo la dhamana namba 13/2007, aliiahirisha kesi hiyo hadi leo, baada ya mshitakiwa kutotokea mahakamani kwa muda uliopangwa.
Awali ombi hilo lilipangwa kuanza kusikilizwa jana saa 5:00 asubuhi, lakini baada ya mshitakiwa kushindwa kutokea kwa wakati, mawakili wake walimuomba Jaji asogeze mbele muda wa kuanza kusikiliza ombi hilo.
Ombi hilo lilikubaliwa na Jaji ambaye aliwaongezea muda hadi saa sita mchana. Hata hivyo, mpaka kufikia muda huo, mtuhumiwa alikuwa hajafika mahakamani, hali iliyosababisha Jaji Mwarija kuahirisha kesi hiyo hadi leo saa tano asubuhi.
Hata hivyo baada ya mahakama kuahirisha ombi hilo, mmoja wa mawakili wa mshitakiwa, Dk. Ringo Tenga, aliwaeleza waandishi wa habari kwamba, mshitakiwa alishindwa kufikishwa mahakamani hapo kwa muda uliopangwa kwa sababu ya kuwapo kwa tatizo la mawasiliano baina ya Polisi na Magereza.
“Polisi kumbe walikuwa hawana taarifa za kwenda kumchukua mteja wetu gerezani Keko na kumleta mahakamani na tatizo hilo tumeligundua saa saba mchana,” alisema Dk. Tenga.
Alisema baada ya kubaini tatizo hilo, waliwasiliana na Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam na walipowataarifu walisema wao (polisi) hawakuwa na taarifa. Hata hivyo, Polisi walifanya jitihada za kumleta na aliwasili mahakamani hapo saa 7:45.
Saa 8:02 mchana gazeti hili lilimshuhudia Ditopile akiwa amekaa ndani ya gari aina na Toyota Balloon, lenye namba za usajili T723 AFD. Ndani ya gari hilo lenye rangi ya fedha, walikuwamo pia askari waliokuwa wamevalia nguo za kiraia, ambao walimleta mahakamani hapo.
Gari hilo halikuegeshwa kwenye lango kuu la mahakama hiyo kama ilivyo kawaida, badala yake liliegeshwa kwenye lango la nyuma linalotumiwa na majaji.
Gazeti hili lilishuhudia baadhi ya ndugu na jamaa wa mshitakiwa wakimsabahi Ditopile ambaye alikuwa ameketi katika kiti cha nyuma.
Ijumaa iliyopita mahakama hiyo ilipanga kusikiliza ombi la dhama hiyo jana, baada ya Ditopile kufunguliwa shitaka la kuua bila kukusudia namba 21/2007.
Katika kesi hiyo, Ditopile anatuhumiwa kumuua dereva wa daladala, Hassan Mbonde, Novemba 4 mwaka jana, majira saa 1:40 usiku, eneo la Lugalo, Dar es Salaam.