EDITH Kahanda na Deo Kahanda, ambao ni mume na mke, wakazi wa Ilala, jijini Dar es Salaam, jana walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakituhumiwa kuuza nyumba ya mirathi kwa sh milioni 115 na kuwadhulumu watoto watatu wa marehemu, Juma Abdallah.
Ilidaiwa mahakamani hapo kuwa Kahanda na mkewe, waliuza nyumba hiyo kwa makubaliano kwamba watawagawia watoto hao fedha hizo lakini hawakufanya hivyo.
Watoto waliodhulumiwa walitajwa kuwa ni Seif Jumbe, Rehema Mashaka na Nusura Abdallah, ambao walidai kuwa kulikuwa na makubaliano ya kulipwa kila mrithi kiasi sawa cha fedha, lakini ikatokea kinyume baada ya waliompendekeza kuwa msimamizi wa mirathi, Edith, kuwadhulumu.
Watoto hao walidai kuwa, Edith aliwaahidi kuwagawia fedha hizo katika kipindi cha wiki mbili tangu kuuzwa kwa nyumba hiyo.
Walidai kuwa wiki mbili zimepita na hawajapatiwa fedha, walifungua shitaka la madai katika Mahakama ya Mwanzo Buguruni, ambayo awali ndiyo iliyomuidhinisha Edith kuwa msimamizi wa mirathi.
Alipofikishwa mahakamani hapo, Edith aliahidi kutoa fedha hizo mara ifikapo Januari 31 mwaka huu. Hata hivyo, hakutoa fedha hizo na watoto hao waliamua kulifikisha suasla hilo mahakamani hapo.
Watoto hao walidai kuwa wakati wanafuatilia fedha zao, mume wa Edith (Deo), aliamua kwenda mahakamani na kudai kuwa mkewe alimuingizia fedha hizo katika akaunti yake katika Benki ya NBC Tawi la Mnazi Mmoja, Dar es Salaam, na kukiri kuzitumia fedha hizo pamoja na mkewe.