HATIMAYE, Jeshi la Polisi nchini, limetamka rasmi kuwa Mbunge wa Buchosa, Samuel Chitalilo (CCM), alighushi vyeti vya elimu yake na aliwadanganya wapiga kura wake.
Limesema, uchunguzi wa kina lilioufanya, umethibitisha pasipo shaka kwamba, Chitalilo hakusoma Uganda, wala jina lake halitambuliki katika Shule ya Sekondari Katikamu, anayodai kusoma, pamoja na kwenye Baraza la Mitihani la nchi hiyo.
Mkurugenzi Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Robert Manumba, aliiambia Tanzania Daima kwa njia ya simu jana kuwa, wamethibitisha Chitalilo ni miongoni mwa wanasiasa wengi waongo, lakini hawezi kushitakiwa kwa sababu elimu si kigezo cha mtu kuwa mbunge.
Alisema polisi walikamilisha uchunguzi wa suala hilo tangu mwaka jana na kulipeka kwa DPP kwa ajili ya hatua zaidi dhidi ya Chitalilo, hata hivyo DPP alilirudisha faili hilo kwa DCI kwa maelekezo kuwa mbunge huyo hana kosa linaloweza kumtia hatiani.
“Ni kweli, uchunguzi wetu umebaini kuwa Chitalilo alisema uongo, alighushi vyeti vyake, hakusoma Uganda, jina lake halipo katika hiyo shule wala katika Baraza la Mitihani la Uganda, lakini ubunge haukuwekewa sifa ya elimu.
“Sisi tulikamilisha uchunguzi wetu mapema tu, tangu mwaka jana, tukapeleka jalada kwa DDP, yeye akatafakari, akaona kisheria hakuna kosa, hawezi kushitakiwa, hivyo akalirudisha faili kwetu kwa maelekezo mengine,” alisema Manumba.
Alisema hatua ilifikiwa kutokana na ukweli kwamba wanasiasa wengi ni waongo, kwamba huwa wanatoa ahadi nyingi kwa wapiga kura wao, lakini hawazitekelezi, hivyo Chitalilo, naye anawekwa katika kundi la wanasiasa wa aina hiyo.
Kamanda Manumba alisema vyombo pekee vilivyobaki, vyenye uwezo wa kuchukua hatua dhidi ya Chitalilo, ni chama chake cha CCM pamoja na taasisi anayoitumikia (Bunge).
Alisema, polisi imekwishafanya mawasiliano ya ndani na vyombo vinavyohusika na viko huru kuchukua hatua yoyote dhidi ya Chitalilo kulingana na taratibu zilizojiwekea.
Manumba alisema CCM ni chama chenye taratibu zake, hivyo wanaweza kuchukua hatua zinazofaa kwa mbunge huyo kama wataona inafaa na Bunge kadhalika nalo lina kanuni na taratibu zake, hivyo Spika anaweza kuchukua uamuzi unaofaa kama itaona inapaswa kufanya hivyo.
Kuhusu wapiga kura wa Buchosa, Manumba alisema polisi wamefanya kazi yao na wameeleza ukweli, hivyo ni jukumu lao kuamua, baada ya kubaini kuwa mbunge wao si mkweli, kutomchagua tena ama kumchagua tena kama wanampenda.
Tanzania Daima ilipowasiliana na Spika wa Bunge, Samuel Sitta kwa njia ya simu jana, simu yake ilikuwa inaita bila majibu, na Katibu Mkuu wa CCM, Yusufu Makamba, simu yake ilikuwa haipatikani.
Madai ya Chitalilo kughushi vyeti vya elimu yake na kuwadanganya wapiga kura wake, yaliibuliwa na mshindani wake kisiasa, Alfred Ngotezi, ambaye alifungua kesi polisi Januari 21, 2006 mjini Sengerema Mwanza.
Kesi hiyo ilipewa namba SEN/IR/104/2006 na katika madai yake, Ngotezi alieleza kuwa, Chitalilo aliwadanganya wapiga kura na vyombo vya dola kuhusu elimu yake wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2005 na 2000.
Alidai kwamba, wakati wa uchaguzi mkuu, Chitalilo alitoa vipeperushi akieleza kuwa yeye ni mhitimu wa kidato cha sita katika Shule ya Sekondari Katikamu nchini Uganda mwaka 1991, na kwamba alihitimu na kutunukiwa stashahada kutoka Manchester Uingereza mwaka 2003, ingawa hakutaja jina la chuo husika.
Waziri wa Usalama wa Raia, Bakari Mwapachu, ambaye aliwahi kuzungumzia kesi hiyo kwa nyakati tofauti katika vyombo vya habari, alikaririwa na gazeti hili akieleza kuwa jarida la kesi hiyo linafanyiwa upelelezi na makachero wa polisi wa makao makuu kwa kushirikiana na polisi wa kimataifa (Interpol).
Mwapachu alikaririwa kwamba amewaagiza polisi kulishughulikia suala hilo haraka na apatiwe taarifa ambazo aliahidi kuziweka hadharani.
Naye Spika Sitta alilizungumzia suala hilo. Alisema kughushi ni kosa la jinai hivyo kama ikibainika kuna mbunge aliyeghushi, sheria itachukua mkondo wake.
Katika hatua ya kushangaza, wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2005, aliyekuwa msimamizi wa uchaguzi wa Sengerema na Buchosa, Sebastian Masso wakati akitoa maamuzi kuhusu pingamizi la mgombea wa NCCR-Mageuzi, Adrian Tizeba alilomuwekea Chitalilo, alisema baada ya kufuatilia madai ya utata wa elimu ya Chitalilo, ameridhika kuwa anayo elimu aliyoijaza kwenye fomu namba 10B (5).
Hata hivyo uamuzi huo wa Masso unapingana na taarifa za upelelezi uliofanywa na polisi kuhusu suala hilo.