MAKAMU wa Rais, Dk. Ali Mohamed Shein, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Abbas Kandoro na Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Kanali Fabian Massawe, jana walishindwa kuhudhuria sherehe za uwekaji wa jiwe la msingi kwa ajili ya ujenzi wa nyumba 63 Mbweni, jijini, zilizoandaliwa na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, John Magufuli.
Kuzuka kwa maneno kuwa Magufuli anatengwa na viongozi wenzake kutokana na ugawaji wa eneo la akiba ya barabara la Rose Garden, kulizidi baada ya Kanali Massawe, kufika eneo la tukio na kuondoka kabla ya kuanza kwa shughuli hiyo.
Kwa mujibu wa mshereheshaji wa shughuli hiyo (MC), wananchi walielezwa kuwa Makamu wa Rais alikwenda kuiwakilisha serikali kwenye mazishi ya askofu mkoani Singida, na badala yake alikuwapo Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Profesa Mark Mwandosya. Kandoro aliwakilishwa na Katibu Tawala (RAC).
Akizungumza katika sherehe hizo, Magufuli alisema serikali ina upungufu wa nyumba milioni mbili na kuifanya nchi kuwa nyuma katika masuala ya makazi na kwamba Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) limebuni mradi wa kujenga na kuuza nyumba kwa kuzingatia uwezo wa wananchi na kuitaka serikali kutenga fedha kwa ajili ya mradi huo.
“Naiomba serikali katika bajeti ya mwaka wa fedha ujayo NHC ipewe ruzuku kutoka serikalini, kwa sababu kazi inazofanya ni za serikali kwa manufaa ya wananchi,” alisema Magufuli.
Alisema shirika hilo linaendelea kujenga nyumba za kuuza katika miji mingi hapa nchini, na sasa imetenga sh milioni 400 kwa ajili ya ujenzi wa maghorofa huko Chalinze, mkoani Pwani.
Kuhusu ujenzi holela, Waziri Magufuli alisema, serikali haitawabomolea wananchi waliojenga kwenye maeneo hayo, badala yake itaweka mazingira ya kuwatambua na kuwapa hatimiliki.
Mradi wa ujenzi na uuzaji wa nyumba Mbweni uko kilomita 35 kutoka jijini Dar es Salaam. Nyumba hizo zimegharimu zaidi ya sh bilioni tatu. Tayari nyumba 15 zimejengwa, kati ya hizo tano zimepata wanunuzi, nyumba moja inauzwa kati ya sh milioni 72 hadi 140 .