RAIS Jakaya Kikwete, amesema matatizo yanayojitokeza katika mikataba mbalimbali ambayo serikali imeingia na wawekezaji, pamoja na mambo mengine, yanasababishwa na uwezo mdogo walionao baadhi ya wataalamu wa Kitanzania wanaoshiriki katika majadiliano ya mikataba hiyo.
Ili kukabiliana na tatizo hilo, Rais Kikwete ameiomba Serikali ya Norway kuwapatia mafunzo na mbinu za kisayansi wataalamu hao zitakazowapa uwezo wa kujadiliana na wawekezaji huku wakiweka mbele masilahi ya taifa.
Alitoa ombi hilo jana Jumatano alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Maendeleo na Ushirikiano wa Norway, Erick Solhein, katika siku yake ya mwisho ya ziara rasmi ya kiserikali nchini hapa.
Alisema Tanzania inawahitaji wataalamu na wakufunzi kutoka Norway kwa kuwa huko nyuma waliwahi kutoa msaada sana wakati wa majadiliano ya mikataba, kiasi cha kuwafanya wakubwa katika taasisi fulani ya Kimataifa ya Fedha kutofurahishwa na umakini ulioonyeshwa kwa upande wa Tanzania.
“Nakumbuka tulipata mtaalamu mmoja mzuri sana kutoka kwenu, alitusaidia kiasi cha kuwaudhi wakubwa wale waliokuwa upande wa wawekezaji na walipoona wanazidiwa kete walimfanyia njama na kumwondoa. Tunawahitaji tena wataalamu kama yule waje kuwafundisha watu wetu,” alisisitiza Rais Kikwete.
Alifafanua kuwa hivi sasa Tanzania inaendelea kufanya ugunduzi wa rasilimali nyingi, zikiwamo za gesi asilia na madini, hali aliyosema kuwa umakini na utaalamu wa hali ya juu unahitajika, ili hatimaye mikataba itakayohusu uendelezwaji wa rasilimali hizo ufanyike kwa umakini na kwa uangalifu mkubwa.
Norway kupitia waziri wake huyo imekubali kulifanyia kazi ombi hilo pamoja na lile la kuisaidia kiuezo na kivifaa Taasisi ya Kuzuia Rushwa (TAKURU).
Katika mazungumzo hayo, waziri huyo alimweleza rais kwamba Tanzania ndiyo nchi inayoongoza kwa kupewa umuhimu wa pekee katika masuala ya misaada ya kimaendeleo kuliko nchi yoyote barani Afrika ukiacha Msumbiji.
Alisema kuwa Tanzania ni nchi iliyo karibu na Norway na kwamba uhusiano kati ya nchi hizo mbili na watu wake haujawahi kutetereka tangu ulipoanza wakati Tanzania ilipopata uhuru wake.
Katika hatua nyingine, akiwa hapa nchini pamoja na kufanya mazungumzo na viongozi wakuu wa serikali na wafanyabiashara, Rais Kikwete pia alikutana na kufanya mazungumzo na Watanzania wanaoishi na kusoma hapa Norway.
Katika salamu zao kwa rais, wanafunzi wa Kitanzania, walisema kuwa wanaunga mkono uamuzi wa serikali kupitia upya majina ya wanafunzi waliopewa mikopo, ili kubaini wenye uhalali na wasio na uhalali wa kupata mikopo hiyo.
Akisoma salamu hizo kwa niaba ya wanafunzi wenzake, John Chalukulu, alisema kuwa pamoja na kuiunga mkono serikali, lakini wanaomba utoaji wa mikopo utolewe kwa asilimia 100 na uwanufaishe wanafunzi wote waliofaulu na wenye sifa za kujiunga na vyuo vikuu.
Wanafunzi hao walilalamikia tabia ya baadhi ya waajiri serikalini ya kutowapatia ruhusa wafanyakazi ambao wamepata ufadhili wa kwenda kusoma. Aidha, walisema kuwa wafanyakazi hao hata pale wanaporejea baada ya kuhitimu mafunzo yao, hawatambuliwi wala kupandishwa vyeo.
Akijibu hoja hizo, Rais Kikwete alisema kuwa atafurahi kama atapewa taarifa za waajiri wa aina hiyo, ili naye aweze kusaidia kulitatua tatizo hilo.
Alielezea kushangazwa na taarifa za kuwapo kwa watendaji serikalini wanaowazuia watumishi wao kwenda kusoma