SERIKALI imevitaka vyombo vya habari nchini kutumia kwa usahihi lugha ya Kiswahili ikiwa ni mbinu ya kukabiliana na ushindani uliopo katika soko la habari duniani.
Rai hiyo imetolewa jana mjini hapa na Waziri wa Habari Utamaduni na Michezo, Muhammed Seif Khatib, wakati wa ufunguzi wa mkutano wa 85 wa waandaaji wa vipindi vya elimu kwa umma kupitia redio na televisheni.
Mkutano huo uliandaliwa na Taasisi ya Utangazaji Tanzania (TUT) kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Khatib, alisema redio na luninga vinapaswa kuepuka lugha za mitaani, badala yake vihakikishe kuwa vinatumia kwa ufasaha lugha ya Kiswahili kama silaha mojawapo ya kuweza kumudu soko la ushindani katika sekta ya habari.
Alisema, kwa kuwa lugha za mitaani zinazotumika kwa baadhi ya redio zimekuwa haziinufaishi jamii, hivyo zisipewe nafasi.
“Hivi sasa kuna baadhi ya redio zinaruhusu matumizi ya lugha za mitaani, hivyo ni kukiharibu Kiswahili, lugha ambayo tunapaswa kujivunia kwani ni lugha ya bara la Afrika na Tanzania ndio waasisi wake,” alisema Waziri Khatib.
Aidha, aliwataka wadau hao kuandaa vipindi hivyo kitaaluma zaidi na kutumia vibwagizo vitakavyotoa ushawishi kwa wengine kuvisikiliza.
Pia alisema mbali na kuwepo kwa matumizi hayo sahihi, waandaaji hao wanapaswa kuwa na mahusiano mazuri na Jeshi la Polisi kwa kuwa wote kwa pamoja wakishirikiana wataweza kutimiza lengo la utolewaji wa elimu hiyo kwa umma.
Nae Mkurugenzi wa TUT, Danstan Tido Mhando, alisema mkutano huo umelenga zaidi kuboresha na kuongeza matumizi sahihi ya lugha ya Kiswahili na kuanzishwa kwa kituo maalumu cha kuhamasisha matumizi ya lugha hiyo.