WAZIRI Mkuu, Edward Lowassa, amemtaka Mwenyekiti wa Chama cha United Democratic (UDP), John Cheyo, kuanzisha sera zake za elimu pale atakaposhinda urais na si kudandia sera zinazotekelezwa hivi sasa na Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Akihutubia mkutano wa hadhara katika Uwanja wa Jamhuri mjini hapa juzi, Lowassa alisema yanayotekelezwa hivi sasa katika elimu, ni matokeo ya mipango na ahadi zilizotolewa na CCM kupitia ilani yake ya uchaguzi katika kampeni za uchaguzi mkuu uliopita.
“Yupo rafiki yetu mmoja mwanasiasa nimemsikia juzi akisema kupita vyombo vya habari kwamba, hii sera yetu isiwabane wananchi kwa kuwalazimisha kujitolea kujenga shule,” alisema Lowassa bila kumtaja Cheyo kwa jina.
Aliendelea kueleza: “Namtaka afahamu kuwa sera hii ni mipango madhubuti tuliyojiwekea na hatukukurupuka tu. Yeye asubiri atakaposhinda ndio aje na sera zake.”
Ingawa hakumtaja kwa jina, lakini mwanasiasa ambaye katika siku za hivi karibuni ametokea katika vyombo vya habari akikosoa sera hiyo ya serikali, ni Cheyo ambaye aliitaka serikali kuacha kuwalazimisha wananchi kuchangia ujenzi wa shule za sekondari, kwani wamekuwa wakifanya hivyo kwa mujibu wa mipango yao waliyojiwekea.
Akielezea zaidi mipango ya serikali kuhusu jambo hilo, Lowassa aliuambia mkutano huo kuwa, Rais Jakaya Kikwete ameidhinisha matumizi ya sh bilioni nane kwa ajili ya kuajiri walimu watakaopangiwa kufundisha katika shule mpya za sekondari zinazojengwa nchini kote.
“Fedha hizo zipo tayari na watu wenye ‘degree’ (shahada) ambazo si za ualimu, lakini wangependa kuwa walimu, tunawakaribisha waombe. Wale waliomaliza kidato cha sita nao wanakaribishwa kuomba na wote hawa watapatiwa ‘crash program’ (mafunzo ya muda mfupi), ili kuwawezesha kuanza kazi mara moja,” alisema.
Alisema, serikali haikukurupuka, imeweka mipango itakayowezesha upatikanaji wa walimu na vifaa vya kufundishia.
“Tunafahamu kuwa ubora wa elimu hautokani na majengo tu, ndio maana tumejiandaa kwa ajili ya kuongeza walimu na vifaa vya kufundishia,” alisema na kuwataka wakazi wa maeneo ambayo walimu wapya watapelekwa, kuwakirimu, ili nao wajione kuwa ni sehemu ya jamii hiyo na kudumu katika utumishi.