Kitaifa
   Siasa
   Jamii
   Uchumi
   Makala

 

Search


Advanced Search

 »  Home  »  Habari za Kitaifa  »  Msafara wa Lowassa wapata ajali Arusha
Msafara wa Lowassa wapata ajali Arusha
By Habari Tanzania | Published  02/26/2007 | Habari za Kitaifa | Unrated
na Mustafa Leu, Arusha

MSAFARA wa Waziri Mkuu, Edward Lowassa, juzi ulipata ajali ukiwa njiani kutoka eneo la Ngurero, mkoani Kilimanjaro kuelekea Monduli, mkoani Arusha.

Ajali hiyo ilitokea saa 11:00 jioni baada ya gari la abiria aina ya Toyota Hiace, lenye namba za usajiri T476 AAT kuligonga gari la polisi aina ya Volks Wagen lenye namba za usajiri STH 1746, lililokuwa likiongoza msafara wa magari ya waziri mkuu.

Habari zilizopatikana kutoka eneo la tukio zilieleza kuwa, chanzo cha ajali hiyo ni kitendo cha dereva wa Hiace inayofanya safari kati ya Arusha mjini na Usa River kupiga kona ghafla kuukwepa msafara wa waziri mkuu, ambaye alikuwa akitokea Moshi katika mazishi ya aliyepata kuwa Mangi Mkuu wa Wachaga, Thomas Marealle (92), aliyefariki dunia zaidi ya wiki moja iliyopita.

Watu walioshuhudia tukio hilo walieleza kuwa dereva huyo ambaye jina lake halikupatikana mara moja alipiga kona kali ghafla baada ya kusikia ving’ora vya polisi vinavyoashirikia kuwapo kwa hali ya tahadhari barabarani.

Tukio hilo lilisababisha, ‘kigofu’ hicho cha polisi kilichokuwa kikiongoza msafara wa Lowassa kuligonga kwa nyuma basi hilo dogo la abiria.

Mara baada ya tukio hilo, majeruhi kadhaa waliohusika katika ajali hiyo walikimbizwa katika Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru.

Daktari Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Dk. Naftali ole King’ori, alisema waliojeruhiwa ni Mkaguzi Msaidizi wa Polisi, Damas Cornel Mzambwe, Sajenti Otto Silvanus Basil na Sajenti Froliani, ambaye alitibiwa na kuruhusiwa kuondoka.

Taarifa zinaeleza kwamba, mara baada ya ajali hiyo, dereva wa Hiace alitoroka kutoka eneo la tukio na kukimbia, na hadi jana alikuwa akiendelea kutafutwa.

Kumekuwa na matukio kadhaa ya ajali yanayohusisha misafara inayokwenda kasi ya viongozi wakuu wa kitaifa katika vipindi tofauti.

Miaka ya mwanzo ya 1990, msafara wa Ali Hassan Mwinyi wakati huo akiwa Rais, ulipata ajali katika makutano ya barabara za Chang’ombe na Mandela Express jijini Dar es Salaam na kusababisha kifo cha aliyekuwa Mkuu wa Polisi wa Kituo cha Chang’ombe.

Mwaka 2000 wakati wa kampeni, msafara wa Benjamin Mkapa aliyekuwa akipigania kuingia ikulu kwa kipindi cha pili, ulipata ajali mkoani Mwanza na kusababisha vifo vya watu kadhaa, baada ya basi moja lililokuwa limeegeshwa pembeni eneo la mlimani kukatika breki na kuanza kuporomoka kwa kasi.


How would you rate the quality of this article?
1 2 3 4 5
Poor Excellent
Add comment
Comments


Article Options
Your Favorite Articles
View All Favorites
Articles to Read
You Recently Viewed...
Popular Articles
  1. Unaifahamu Jambo Forums?
  2. Barua ya Wazi kwa Rais Jakaya Kikwete
  3. Ghorofa Jijini lanusurika kuungua moto
  4. Is Tanzania a safe place to invest?
  5. Britsh M.P. calls for the suspension of aid to Tanzania.
No popular articles found.
Popular Authors
  1. Habari Tanzania
  2. Mzee Mwanakijiji
  3. Marshy Abdu
  4. Linda Garner
  5. Nthelezi Nesaa
  6. Prosper Kwigize
  7. Ramadhan Semtawa
  8. Salehe Mmoro
  9. Manyerere Jackton
  10. Ndesanjo Macha
No popular authors found.