Na Mwandishi Wetu, Mwanza
SERIKALI imewahimiza raia wa nchini zilizomo kwenye Bonde la Mto Nile kulinda, kutumia vizuri na kuendeleza rasilimali zake kwa manufaa ya nchi hizo na vizazi vijavyo.
Akizungumza kwenye maadhimisho ya Siku ya Nile iliyofanyika Kijiji cha Nyashimo wilayani Magu juzi, kwa niaba ya Waziri wa Maji Dk Shukuru Kawambwa, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Dk James Msekela alisema kuwa, raia hao, wanapashwa kutumia vizuri na kuziendeleza rasilimali hizo kwa kwa manufaa yao wenyewe.
Dk Kawambwa alisisitiza kuwa, hatua hiyo itasaidia na kufanikisha maendeleo ya kiuchumi katika nchi hizo kumi zinazotegemea bonde hilo katika masuala mbalimbali ya kijamii.
Nile una rasilimali nyingi ambazo hazijatumika kikamilifu pia zipo ambazo zinawanufaisha wananchi, hivyo kuufanya mto huo, uwe endelevu unaohitaji kuhifadhiwa.
Pamoja na rasilimali nyingi kutotumika katika bonde hilo, lakini wananchi wengi wanaolizunguka ni maskini duniani, wanasumbuliwa na magonjwam hawana uhakika wa maji safi na salama kwa kunywa na matumizi ya nyumbani, pia wanakipato kidogo.
Wananchi hao, wanakabiliwa na matatizo ya umeme, ukame na hawana uhakika wa chakula kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa duniani.
Mabadiliko hayo ya hali ya hewa yanatokana na mazingira yanayotuzunguka milima, misitu, maziwa kuharibiwa huku , ardhi yenye rutuba ikipotea ,wanyamapori kupungua na uchumi kuwa dhaifu na kusababisha vijana kukosa ajira.
Wakati hayo yakitokea, idadi ya watu nayo inazidi kuongezeka, hivyo kufanya matumizi ya rasilimali nayo kuongezeka.
Tanzania inashirikiana na nchi nyingine katika umiliki, utunzaji na matumizi ya rasilimali ya maji ili kuweza kushirikiana katika kuondoa umaskini, njaa, magonjwa,uhaba wa nishati na mmomonyoko wa udongo.
Hatua hiyo ilizifanya nchi hizo, ziunde Nile Basin Inititave (NBI), kufanikisha maendeleo ya kiuchumi, kijamii kwa kuzingatia matumizi endelevu yanayozingatia usawa na faida zitokanazo na rasilimali maji ya bonde hilo.