Na Mwandishi Wetu
MAKAMU wa Rais, Dk Ali Mohamed Shein, amesema Tanzania inatambua mchango unaotolewa na Kanisa la Orthodox katika kusaidia utekelezaji wa miradi ya maendeleo nchini.
Dk Shein alitoa kauli hiyo jana, alipokutana na Kiongozi Mkuu wa Kanisa hilo duniani, Papa Theodoros Ikulu Jijini Dar es Salaam alikokwenda kumsalimia.
Alisema misaada inayotolewa na kanisa hilo katika sekta za afya, elimu na maji katika baadhi ya miji nchini, inasaidia jitihada za serikali katika kuhakikisha wananchi wake wanapata huduma hizo kwa uhakika tena karibu na maeneo wanayoishi.
Aidha Makamu wa Rais alielezea nia ya serikali ya kuweka mazingira mazuri ya uwekezaji na kutoa wito kwa kanisa hilo kuendelea kuwekeza nchini Tanzania, hasa katika sekta ya elimu
Katika mazungumzo hayo, Papa Theodoros aliipongeza Tanzania kwa kuweka mikakati madhubuti ya kuwaletea wananchi wake maendeleo endelevu kwa upande wa uchumi na masuala ya kijamii.
Alisema katika programu yake ya utekelezaji wa miradi ya jamii barani Afrika, Tanzania itakuwa miongoni mwa nchi zitakazopewa kipaumbele ili iweze kufanikisha azma yake ya kuleta maisha bora kwa wananchi.
Papa huyo kesho anatarajia kwenda mkoani Iringa ambako atazindua kituo cha afya cha kwanza kilichojengwa na kanisa hilo . Kituo hicho kinategemewa kuhudumia wananchi wa vijiji tisa vya mkoa huo.