Na Gasper Andrew
SERIKALI imeombwa kuangalia uwezekano wa kuongeza idadi ya vituo vya kutolea huduma
ya dawa za kurefusha maisha (ARV), ili visaidie kuhudumia wagonjwa wengi zaidi wa
ukimwi mkoani Singida.
Wito huo umetolewa na Mratibu wa Mpango Kudhibiti Maambukizi ya Virusi vya Ukimwi, mkoani Singida, Dk Khalid Msangi wakati akizungumza katika warsha ya kuweka mkakati wa kupambana na ugonjwa huo.
Alisema takwimu zinaonyesha kuwa zaidi ya watu 35,000 wameambukizwa virus vya ukimwi tangu ugonjwa huo uingie mkoani Singida mwaka 1986.
Dk Msangi alisema pamoja na idadi hiyo kubwa, ni wagonjwa 1,769 tu waliojitokeza
kwenye vituo vya hospitali za Mkoa, Manyoni, Iramba, Itigi na Makiungu na kupatiwa dawa za kurefusha maisha.
Mratibu huyo alisema hali hiyo inasababishwa na idadi ndogo ya vituo na kutofikika kwa urahisi kutokana na umbali.
Kutokana na hali hiyo, Dk Msangi alisema kuna haja kwa serikali kuhakikisha kuwa
huduma hizo zinasogezwa hadi kwenye vituo vya afya na zahanati za vijijini, ili kuwafikia waathirika wengi zaidi wa ukimwi.