Na Waandishi Wetu
MIEZI miwili baada ya mabilioni ya fedha za kuwawezesha wananchi zilizotolewa na serikali ya awamu ya nne kuingia katika benki, bado fedha hizo zimekwama katika benki za CRDB na NMB kutokana na wakopaji wengi kukosa sifa.
Chanzo kikubwa cha wakopaji wengi kukosa sifa ni hamasa zinazotolewa na wanasiasa kwa wananchi katika maeneo yao, wakiwahamasisha kwenda kukopa, bila kuwafafanulia ni kitu gani hasa kinachotakiwa kwa mtu au taasisi inayotaka kuomba mkopo wa fedha hizo.
Uchunguzi uliofanywa na Mwananchi katika mikoa kadhaa nchini, umeonyesha kuwa maombi mengi yaliyotumwa na vikundi vya wajasiriamali pamoja na watu mmoja mmoja kuomba fedha hizo, yamekwama kutokana na kukosa sifa zinazotakiwa na benki.
Vile vile, kikwazo kingine ni wanasiasa kutoa taarifa zisizo sahihi kwa wananchi kuwa fedha hizo zinatolewa bure bila ya masharti yoyote, hali ambayo imesababisha watu kwenda benki kuomba mikopo hiyo bila ya kuelewa taratibu zinazotakiwa kufuatwa.
Inaelezwa pia kuwa elimu duni miongoni mwa wananchi juu ya namna ya kuzipata fedha hizo, imesababisha watu wengi kushindwa kutuma maombi ya mikopo katika benki hizo mbili, zilizokabidhiwa jukumu la kusimamia utoaji wa mikopo hiyo kwa wananchi.
Mkurugenzi wa Benki ya CRDB moja ya benki ambazo zimepewa fedha za serikali kutoa mikopo kwa wananchi, Dk. Charles Kimei aliiambia Mwananchi jana kuwa benki yake imepata sh bilioni 5.25 na serikali kwa ajili ya kutoa mikopo ya uwezeshaji.
Hata hivyo, alisema mikopo hiyo itatolewa kwa vikundi au vyama vya kuweka na kukopa ambavyo vinakidhi vigezo vya benki ili kuhakikisha kuwa fedha zinazotolewa hazipotei.
Alisema lengo la fedha hizo ni kuhakikisha kuwa anayekopa anarejesha mkopo wake ili watu wengine waweze kukopa pia.
Dk Kimei alisema kama kuna watu ambao wanaona kuwa kuna urasimu au cheleweshaji wa mikopo hiyo kupitia benki yake ni kwamba taratibu kadhaa lazima zifuatwe kabla ya kutolewa mikopo hiyo.
Alisema moja ya taratibu hizo lazima saccos mabayo itaomba mkopo ya fedha kupewa mafunzo ya nanma ya kuzitumia ili kuwepo uhakika wa kuzirejesha.
Mkurugenzi huyo alisema benki yake haiwezi kuzitoa fedha hizo bila ya kufuata taratibu na kwamba wanaoingiza siasa za kueleza kuwa fedha hizi zinatolewa bure bila ya masharti wanakosea.
Kutoka Tanga Burhani Yakub, anaripoti kuwa fedha zilizotolewa na Serikali kwa ajili ya mikopo kwa vikundi vya wajasiriamali Wilaya ya Tanga, zimekosa wakopaji kutokana na wananchi kushindwa kuhamasika kuziomba.
Hadi mwanzoni mwa wiki hii, benki ya CRDB ilikuwa bado haijapokea maombi yoyote ya mkopo kutoka kwa vyama vya kuweka na kukopa (Saccos) zilizopo katika Manispaa ya Tanga.
Hata hivyo, Benki ya NMB tawi la Madaraka hadi sasa imepokea maombi 11 tu ya kutaka kukopeshwa fedha hizo, lakini yote yakikumbana na kisiki cha kukosa vigezo vinavyotakiwa.
Kaimu Meneja wa CRDB Tawi la Tanga, Richard Mkakala, alisema wiki hii kuwa benki hiyo, ambayo imepewa jukumu la kushughulikia utoaji mikopo kwa vyama vya akiba na mikopo (Saccos), hadi jana ilikuwa haijapokea maombi kutoka vyama.
“Hadi sasa hatujapokea ombi hata moja la mkopo wa kutoka mfuko wa bilioni moja za wananachi, bado tunaendelea kushirikiana na vyombo vingine katika mchakato wa kutoa elimu kwa wananchi ili waje kuomba kupitia Saccos,” alisema Mkakala na kutolea mfano kuwa wakati akizungumza na Mwananchi, Afisa anayeshughulikia mikopo katika benki hiyo alikuwa kwenye mkutano na wataalamu wa Halmashauri ya Jiji.
Akitoa ufafanuzi zaidi, Kaimu Meneja huyo alisema Saccos pekee ambazo zimekuwa zikinufaika na benki hiyo hata kabla ya kutolewa kwa fedha hizo Serikali ni 10 wakati zilizofanikiwa kukopeshwa ni nne pekee zikisimamiwa chini ya kitengo chake cha Microfinance.
Naye Kaimu Meneja wa NMB Tawi la Madaraka, Mwajombe Fabian, alisema hadi jana, ni maombi 10 tu kutoka vikundi vya kata ya Ngamiani na kimoja cha Kata ya Mzizima Jijini hapa, ndivyo vilikuwa vimewasilisha maombi ya fedha hizo za Seriakli.
Hata hivyo, Mwajombe ambaye pia ni Mhasibu wa benki hiyo, aliyekuwa akizungumzia maombi ya Jiji la Tanga pekee kutokana na wilaya nyingine kuwa na matawi ya NMB, alifafanua kuwa vikundi hivyo vyote vimerejeshewa maombi hayo ili viweze kukamilisha vigezo vinavyohitajika.
“Vikundi vinaleta maombi ambayo yapo tofauti na maelekezo ya utoaji mikopo hiyo, wanaomba kwa shughuli za biashara wakati maelekezo ni kuvikopesha vikundi vyenye michanganuo ya kuendesha shughuli za uzalishaji mali,” alifafanua Mwajombe.
Alisema benki hiyo, ambayo imeelekezwa kukopesha vikundi, mtu mmoja mmoja na vyama vya akiba na mikopo, imengundua kuwa elimu ya mikopo hiyo bado haijaelekezwa kwa walengwa na hivyo imeamua kushirikiana na vyombo vingine kuwaelimisha wananchi ili wawe na uhakika na wanachoomba.
Akitoa melezo juu ya mikopo hiyo, Afisa Ushirika wa Jiji la Tanga, Kungube Misalaba, alisema hadi jana ni vyama 31 vilivyokuwa vimesajiliwa, 13 kati yake vikiwa ni vipya ambavyo vilijisajili baada ya zaiara ya Waziri Mkuu, Edward Lowassa mkoani Tanga, mwishoni mwa mwaka jana.
Alisema idadi hiyo ni mbali ya vikundi vya uzalishaji mali na mtu mmoja mmoja ambao kimsingi wanaruhusiwa kuomba mikopo hiyo na kwamba vyama vya akiba na mikopo kutoka katika vijiji vya Wilaya ya Tanga ni vitatu vya kata za Pongwe na Mabokweni.
Alisema hadi sasa vyama na vikundi hivyo havijaanza kukopa fedha hizo kwa kuwa ofisi yake inasubiri maelekezo kutoka wizarani.
Alisema kutokana na utaratibu uliopo ,anaamini kwamba ifikapo wiki ya pili ya mwezi Machi, mikopo hiyo itaanza kutolewa rasmi kwa walioomba na akafafanua kuwa hivi sasa ofisi yake inaendesha semina za elimu kwa wataalamu, viongozi wa kata, mitaa, vijiji na vitongoji ili kuwawezesha wananchi kupata ufahamu wa namna ya kuomba fedha hizo.
Kutoka Bukoba, Lilian Lugakingira, anaripoti kuwa Sh1 bilioni zilizopelekwa na serikali mkoani Kagera kwa ajili ya kuwakopesha wajasiriamali, zimekosa wakopaji wenye sifa.
Fedha hizo, zimepitishiwa Benki ya CRDB mkoani hapa, lakini hadi sasa hakuna watu binafsi au kikundi ambacho kimetimiza sifa na vigezo vya kukopeshwa.
Meneja wa CRDB, Tawi la Bukoba, Steven Mgwagi aliwaambia waandishi wa habari kuwa tatizo kubwa lililojitokeza ni ukosefu wa elimu ya kutosha kuhusiana na taratibu za utoaji wa mikopo hiyo.
Awali, meneja huyo alisema fedha hizo ziliingizwa kwenye tawi lake tangu Desemba mwaka jana na mpaka sasa ni Saccos moja tu ya walimu iliyojitokeza kuomba fedha hizo, lakini akasema benki imeshindwa kuipata kwa kuwa haipo miongoni mwa Saccos zinazotakiwa kukopeshwa.
Hata hivyo alisema pamoja na Saccos hiyo kutopatiwa mkopo kutoka katika fedha serikali, walimu hao watapatiwa mkopo kutoka katika mfuko maalum wa benki hiyo.
"Hata wale ambao huja kama vikundi, unakuta kuna mambo ambayo hawajakamilisha, hivyo benki huwashauri kukamilisha taratibu ndipo warudi kupatiwa mikopo, lakini wakienda hawarudi... tataizo hilo linatoka na jamii kutopatiwa elimu mapema juu ya mikopo hiyo," alisema
Mgwagi alionya kuwa, kama serikali haitakuwa na mpango maalum wa kuelimisha wananchi jinsi ya kutumia fedha hizo, lengo la serikali la kupunguza umaskini hasa kwa wananchi wa hali ya chini halitafanikiwa.
Kutoka Manispaa ya Temeke jijini Dar es Salaam, James Magai anaripoti kuwa
wakati wananchi mbalimbali wanaojitokeza kuomba mikopo hiyo wakilalamikia kuwepo kwa mizengwe katika taratibu za utoaji mikopo hiyo kwa kile wanachokiita masharti magumu yanayotoelewa na benki, Afisa Ushirika wa Manispaa ya Temeke, Jennifer Katua, ametetea msimamo wa benki hizo.
Akizungumza na Mwananchi ofisini kwake mwishoni mwa wiki, Katua alisema benk hizo hazistahili kulaumiwa kwa msimamo wake juu ya taratibu za utoaji mikopo hiyo na kuwa ziko sahihi na badala yake alisema tatizo liko kwa viongozi kutokuwaeleza wazi wananchi juu ya taratibu za kupata mikopo hiyo.
“Tatizo linalojitokeza katika mikopo hiyo ni kwamba siasa zinaingia mno. Viongozi hawawaelezi wazi wananchi taratibu sahihi za kupata mikopo na badalan yake wanawaambia tu kuwa mikopo hiyo inatolewa bure bila kuwaeleza taratibu za kibenki," alisema Katua.
Alisema kabla ya kuanza kutoa mikopo hiyo, ilitakiwa wananchi waelimishwe juu ya taratibu za kupata mikopo pamoja na mbinu za kuendesha biashara.
Katua alisema unafuu wa mikopo hiyo ni kulegezwa kwa masharti ya dhamana tu na mlolongo wa taratibu za kufikia kupata mikopo hiyo, lakini taratibu nyinge za kibenki ziko pale pale na kwamba viongozi wanatakiwa wawaeleze wananchi waziwazi.
Katua alisema wananchi ambao maombi yao hayakubaliwi na benki hizo ni wale ambao hawako katika kikundi au ushuirika wowote uliosajiliwa wala hawana leseni za biashara, ambavyo ndivyo vigezo vikuu vya kupata mkopo. Hata hivyo alisema ili mwanachama katika ushirika wowote aweze kupata mkopo, lazima awe ametimiza siku tisini tangu kujiunga na ushirika huo.
Akizungumzia mwitikio wa wananchi katika Manispaa hiyo juu ya mikopo, alisema wananchi wengi wamekuwa wakimiminika ofisini kwake kupata elimu ya mikopo hiyo, lakini alipotakiwa kuleza idadi ya maombi yaliyokwisha wasilishwa ofisini kwake, alisema hadi siku hiyo alipokuwa akizungumza na gazati hili hapakuwa na maombi yaliyokuwa yamewasilishwa ofisini hapo.
“Mambi yanayopitia hapa ni ya vikundi vya ushirika tu ambavyo ndivyo tunavyoshughulika navyo, lakini maombi ya watu binafsi taratibu zao zinaishia katika serikali za mitaa na sisi wanatuletea taarifa tu za maombi yaliyowasilishwa na yaliyokubaliwa na benki kupewa mikopo,” alisema na kuongeza;
“Kwa upande wa wanachama wetu, mpaka sasa kuna Saccos mbili tu ambazo zimejitokeza kuomba mikopo. Hata hivyo bado nazo hazijawasilisha maombi rasmi kwani bado zinakamilisha taratibu za kibenki kwanza.”
Kutoka Manispaa ya Ilala, Abeid Poyo anaripoti kuwa Manispaa hiyo imepitisha maombi 787 kutoka kwa wananchi wa manispaa hiyo.
Akizungumza na Mwananchi, Mratibu wa Mpango wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi kupitia Mikopo yenye Masharti Nafuu wa Manispaa, Ellioth Mwasabwite, alisema maombi hayo, yanayojumuisha vikundi na watu binafsi, yametoka katika ngazi ya kata na sasa yapo katika ngazi ya benki.
Alizitaja kata ambazo hadi Februari 9 zilikwisha peleka mchanganuo wa waombaji mikopo kuwa ni Segerea waombaji 731 na Ukonga waombaji 56.
“ Licha ya kuwa hatujawasilana bado na maafisa watendaji wa kata nyingine kujua idadi kamili lakini wananchi wengi wamehamasika na kujitokeza kuomba mikopo,” alisema.
Mwasabwite aliongeza kuwa hamasa ya wanachi kuomba mikopo imetokana na mafunzo elekezi ambayo ofisi yake iliwapa madiwani, maafisa watendaji wa kata, wenyeviti wa mitaa na maafisa wengine ambao walikuwa na jukumu la kuwafikishia wananchi elimu sahihi juu ya mikopo hiyo.
Wakati huo huo, Mwasabwita ameliambia gazeti hili kuwa ofisi yake imelifanyia kazi na kulitatua tatizo la mawasiliano lililojitokeza mwanzoni mwa wiki iliyopita kati ya waombaji mikopo na uongozi wa benki ya NMB tawi la Ilala.
Waombaji hao ambao ilibidi waandamane hadi ofisi za mkoa, walidai maafisa wa benki hiyo waliwapa maelezo na masharti tofauti na yale waliyoyapata kutoka kwa viongozi wao wa manispaa.
Alisema maelezo na masharti yaliyowakanganya waombaji yalikuwa waombaji kutakiwa kuwa na leseni za biashara na dhamana. Pia benki iliwaambia isingetoa mkopo wowote utakaohusu sekta ya kilimo au mifugo.
Kuhusu leseni, ilikubaliwa kuwa mwombaji wa mkopo wa chini ya Sh500,000 hatalazimika kuwa na leseni wakati mwombaji katika sekta ya kilimo au mifugo atalazimika kuomba mkopo kupitia Saccos.
Kuhusu dhamana, alisema kulikuwa na dosari katika tangazo la benki kwa wananchi kwani katika mikopo ya serikali, wananchi hawahitajiki kuwa na dhamana ya aina yeyote na kuwa jukumu hilo ni la serikali.
Naye Jonas Songora anaripoti kutoka Kinondoni kuwa taratibu zilizowekwa na benki ya NMB zimeelezwa kuwa chanzo cha malalamiko ya wananchi wa eneo la Kinondoni jijini Dar es Salaam,hivyo kusababisha kunyimwa fursa ya kupewa fedha za mkopo.
Afisa Ushirika wa Manispaa ya Kinondoni,Ramadhani Bukuku akizungumza na gazeti hili ofisini kwake, alisema kuwa taratibu za kibenki zinawakwamisha watu wengi wanaojitokeza kuomba mikopo hiyo hata baada ya maombi hayo kupitishwa katika ngazi ya wilaya.
Uongozi wa benki unataka kupewa leseni ya biashara kwa watu, vikundi wanaotaka kupewa mikopo hiyo jambo ambalo linapingana na mwongozo wa serikali unaoeleza kuwa mikopo hiyo itolewe kwa wananchi kwa masharti nafuu kwa nia ya kuwawezesha masikini kujikwamua kiuchumi.
"Serikali ilishafuta utoaji wa leseni kwa wafanyabiashara ndogondogo kama mamantilie,wafugaji na wauza mkaa hivyo kunyimwa kwao hadhi ya kupata mkopo huleta usumbufu,kwani hurudi tena ofisini kwangu nakuanza kutoa malalamiko yao katika ofisi zetu,"alisema Bukuku.
Hata hivyo, Bukuku alisema kuwa maombi ya baadhi ya Sacoss yamekwisha pelekwa katika benki ya CRDB na utaratibu unaendelea ili kupata ukomo wa madeni (2007) kutoka kwa Mrajisi Msaidizi wa Vyama vya Ushirika mkoa, ambaye ndiye anahusika na kutoa vibali hivyo.
Alizitaja Sacoss hizo ambazo zimepitishwa katika ngazi ya wilaya Kinondoni ambazo maombi yake yanashughulikiwa na benki ya CRDB kuwa ni Kimara Youth, Kidiyosa, Shekilango Touth, Manzese, Mbezi Beach, Bunju Community.
Juhudi za kumpata Meneja wa benki ya NMB Tawi la Kinondoni aliyejulikana kwa jina moja tu la Kimweri kuelezea kuhusu taratibu hizo zinazolalamikiwa na wakazi wa Kinondoni hazikufanikiwa baada ya kuelezwa kuwa hayupo ofisini kwake.
Naye Richard Kilumbo, anaripoti kutoka Kyela kuwa baadhi ya Wananchi katika maeneo mbalimbali wilayani Kyela, mkoani Mbeya, wamelalamikia utoaji mbovu wa fomu za maombi ya mkopo, wakidai kuwa katika maeneo mengi, fomu hizo zimetolewa kwa upendeleo na wengine kuzipata baada ya kutoa chochote.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika vijiji mbalimbali, wananchi waliokutwa katika ofisi mbalimbali za vijiji katika kata za Kyela Mjini, Ipinda, Mwaya, Makwale na Matema, walilalamikia vitendo vilivyokuwa vikifanywa na baadhi ya maafisa watendaji na wenyeviti wa vitongoji katika maeneo hayo kutoa fomu kwa upendeleo.
Walidai kuwa baadhi ya watendaji wamekuwa wakiuza fomu hizo kuanzia Sh500 hadi Sh1,000 na wakati mwingine kuzitoa kwa upandeleo kwa baadhi ya familia.
Hata hivyo, baadhi ya maafisa watendaji waliozungumzia tuhuma hizo, walisema walichokifanya ni kuzigawa fomu hizo kwa wenyeviti wa vitongoji ambao nao walipaswa kuwagawia mabalozi wa nyumba kumi ili waweze kuwapatia wananchi kwa urahisi.
Walisema ni vigumu kwao kubaini kama fomu hizo zilikuwa zikiuzwa ama kutolewa kwa upendeleo na wakalaani tabia ya baadhi ya wananchi kupenda kulalamikia nje badala ya kupeleka malalamiko hayo katika ofisi zao ikiwa na kuwataja wanaohusika kufanya vitendo hivyo.
Hivi karibuni, Mkuu wa Wilaya ya Kyela, Mashimba Hussein Mashimba, aliwaonya viongozi wa mitaa kuwa yeyote atakayebainika kuwa ametoa fomu hizo kwa upendeleo, atachukuliwa hatua za kinidhamu.
Naye Samuel Msuya anaripoti Morogoro kuwa baadhi ya wananchi mkoani hapa, wamewalalamikia wenyeviti wa mitaa kuwa wanawakwamisha kupata fedha za mikopo zilizotolewa na serikali kwa ajili ya kuwakwamua katika umasikini.
Wakizungumza mjini hapa kwa nyakati tofauti, wananchi hao walisema wamekuwa wakikutana na vikwazo vingi kwa wenyeviti wa mitaa kiasi cha kuwakatisha tamaa ya kupata fedha hizo.
Mmoja wa wananchi hao, Selemani Mkoba , ambaye ni mfanyabiashara ndogo ndogo katika soko la Mawenzi, alisema pamoja na uongozi wa manispaa ya Morogoro kuwahimiza kuzichangamkia fedha hizo, lakini amekatishwa tamaa na mwenyekiti wake wa mtaa.
Mfanyabiashara huyo ndogo ndogo alisema juhudi zake za kupata fomu ya mikopo hiyo kutoka kwa mwenyekiti wa mtaa wake zimekwama kwa kile kilichodaiwa amekuwa hahudhulii vikao mtaa.
Mwananchi mwingine aliyejitambulisha kwa jina moja la God, alidai kuwa wenyeviti wengi wa mitaa wamekuwa wakiwapa vipaumbele wafanyabiashara wakubwa katika kupitisha fomu zao.
Alisema kutokana na hali hiyo, huenda mkakati wa serikali wa kuwainua kiuchumi wananachi wake kupitia fedha hizo ukakwama kama juhudi za haraka hazitachukuliwa kuondoa kasoro hiyo.
"Naomba Manispaa na Serikali Kuu kuliangalia kwa undani suala hili vinginevyo fedha hizo zitawanufaisha zaidi wafanyabiashara wakubwa na kutuacha sisi tukiendelea kuumia na umaskini," alisema God
Wakati hayo yakitokea, hivi karibuni Manispaa ya Morogoro iliwataka wananchi kujitokeza kwa wingi kuomba fedha hizo, ambazo walisema hazina riba kubwa.
Kutoka Dodoma, Michael Uledi, anaripoti kuwa wakazi 20 wa Kata ya Makutupora nje kidogo ya mji wa Dodoma, wamekabidhiwa awamu ya kwanza ya mikopo ya sh milioni 15.8 na Benki ya NMB ikiwa ni utekelezaji wa mpango wa Rais Jakaya Kikwete kuwasaidia wazalishaji wadogo kujiinua kiuchumi.
Fedha hizo zilikabidhiwa na Mkuu wa Mkoa, William Lukuvi, katika uzinduzi wa utoaji wa mikopo hiyo iliyotolewa na benki hiyo kwa watu binafsi.
Akizungumza katika hafla hiyo, Lukuvi aliwataka wakazi wa Mkoa wa Dodoma kuzichangamkia fedha hizo kwa ajili ya kukabiliana na tatizo sugu la ukosefu wa mitaji ambalo limechangia umaskini miongoni mwa watu.
Lukuvi alisema fedha hizo zinalenga kusaidia Watanzania kujiongezea kipato na kuwataka wafahamu kuwa hazitatolewa kwa kuzingatia itikadi ya chama, jinsia na ama ubaguzi wa aina yoyote.
Lukuvi alielezwa kushangazwa kwake na uchamfu ulioonyeshwa na Kata ya Makutupora iliyo nje ya mji, ikizishinda kata nyingine kadhaa zilizopo katikati ya mji wa Dodoma.
Mkuu huyo wa Mkoa aliitaka NMB tawi la Dodoma kuhakikisha inaongeza kasi ya kushughulikia maombi ya mikopo ili wananchi wengi zaidi wanufaike na mpango huo.
Awali Meneja wa NMB kanda ya magharibi, Augustino alisema katika uzinduzi wa utoaji mikopo hiyo, watu hao 20 walipewa fedha hizo walizoomba na kwamba uzinduzi huo unalenga kuwahamaisha wajasiriamali mkoani hapa kujitokeza kuomba mikopo hiyo.
Augustino alisema hadi wiki iliyopita, NMB Dodoma ilikuwa imepokea maombi 128 kwa ajili ya mikopo hiyo na kwamba fedha hizo zinatolewa kwa wajasiriamali kwa kuzingatia masharti yaliyokubaliwa baina ya NMB na Serikali, ingawa alisema imedhihirika kuwa kuna baadhi ya waombaji wanaofanya udanganyifu.
Alisema kuwa kasoro nyingine ni pamoja na michanganuo mingi kutokamilika na kwamba wengi wa wajasiriamali wanaomba fedha nyingi zaidi ya uwezo wa biashara zao na hivyo kukwamisha kasi ya utoaji mikopo hiyo