MUFTI wa Tanzania, Sheikh Mkuu, Sheikh Issa bin Shaaban Simba, amemfuta kazi ya ukurugenzi wa dini katika Baraza la Waislamu wa Tanzania (BAKWATA), Sheikh Suleiman Gorogosi na wakurugnzi wengine wanne.
Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa juzi na Mwenyekiti wa Taifa wa BAKWATA, Sheikh Khamis Mataka, ilieleza kuwa mabadiliko hayo yametokana na mchakato wa kujipanga upya kwa ajili ya kuutumikia Uislamu.
Akitangaza mabadiliko hayo wakati wa kikao cha wakurugenzi mbalimbali wa BAKWATA, juzi, Mufti Simba, alisema ameazimia kutekeleza maoni ya Waislamu wanaolitegemea baraza hilo kwa ajili ya maendeleo yao na taifa.
Alisema kuwa, viongozi hao wataendelea kuwa wafanyakazi wa baraza, huku wakisubiri kupangiwa kazi nyingine chini ya mfumo mpya wa utendaji (MMU), wenye lengo la kuboresha huduma za baraza hilo.
Pamoja na Gorogosi, wakurugenzi wengine waliofutwa kazi na vyeo vyao kwenye mabano ni Mohamed Mvogogo (Elimu na Mafunzo ya Ufundi), Suleiman Lolila (Afya), Twaha Majaliwa (Naibu Mkurugenzi wa Dini) na Ramadhan Samamba (Usalama).
Baada ya kikao hicho, Mufti aliwaagiza wakurugenzi hao kukabidhi ofisi na majukumu yote kwa Kaimu Katibu Mkuu, Sheikh Hassan Luambano, atakayesimamia shughuli zote za kurugenzi hizo.
Aidha, katika kikao hicho, Mufti ameahidi kutangaza mfumo huo mpya (MMU) hivi karibuni na kuwashukuru wakurugenzi waliotolewa madarakani kwa ufanisi wao kwa kipindi chote walicholitumikia baraza hilo.