FEDHA za serikali zilizotengwa kwa ajili ya kusaidia ujasiriamali mkoani Arusha, bado zinaendelea kubakia katika Benki ya CRDB, zikisubiri halmashauri ya manispaa hiyo kuwasilisha orodha ya vikundi na vyama vya akiba na mikopo (SACCOS) vilivyopatiwa mafunzo.
Meneja wa CRDB Mkoa wa Arusha, Chiku Issa, alisema hadi jana benki yake ilikuwa haijapata orodha ya vikundi hivyo, jambo ambalo linaifanya ishindwe kutekeleza kwa vitendo mpango wa serikali wa kuwawezesha wananchi kiuchumi.
Benki hiyo pamoja na NMB, ndizo zimepewa dhamana ya kusimamia fedha hizo katika Mkoa wa Arusha zilizobatizwa jina la ‘Mabilioni ya Kikwete’.
Akihojiwa ofisini kwake jana, Chiku alisema, anadhani halmashauri zimeshindwa kuendesha mafunzo katika ngazi za kata na vijiji, juu ya namna ya kusimamia fedha hizo.
Alibainisha kuwa, benki hiyo hutoa mikopo hiyo kupitia SACCOS ama vikundi, kutegemea mahitaji ya chama husika, kwani fedha hizo zinahitaji uadilifu na nidhamu ya hali ya juu katika kusimamia matumizi na marejesho, ili wananchi wengine waweze kukopeshwa kupitia vikundi ama SACCOS zao.
Chiku alisema, inaelekea asasi za kifedha katika ngazi ya kata na vijiji, bado hazijawezeshwa kwa kupatiwa mafunzo ama kuelimishwa, ili wananchi ambao ni wanachama wake, waweze kukopeshwa kutoka mfuko huo wa Rais Kikwete.