SASA ni dhahiri kwamba, kuna kila dalili kwa aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Ukiwaona Ditopile-Mzuzuri kutoka katika mahabusu ya Keko alikokaa kwa takriban miezi mitatu sasa.
Uwezekano wa hilo kutokea, unatokana na ukweli kwamba, wakati wowote kuanzia sasa, mwanasiasa huyo anaweza akaanza kujibu mashitaka ya kuua bila kukusudia ambayo kisheria yana dhamana.
Habari zilizoikariri Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka ya Jinai na ambazo jana zilithibitishwa na Msajili wa Wilaya Kanda ya Dar es Salaam, Phophir Lyimo, zinaeleza kwamba, jalada la shauri hilo la Ditopile limeshawasilishwa Mahakama Kuu, ambayo kisheria ndiyo yenye mamlaka ya kusikiliza kesi zote za mauaji.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, Lyimo, alisema jalada hilo lilifikishwa hapo na kupokelewa Januari 31, mwaka huu.
Lyimo, alieleza pia kwamba, hati ya mashitaka ya Ditopile, ambaye akifikishwa hapo atakuwa akikabiliwa na mashitaka ya kuua bila kukusudia, imeshapewa namba 13/2007.
Kukamilika kwa upelelezi wa polisi kuhusu shauri hilo la Ditopile, ambaye anatuhumiwa kutenda kosa la kumuua dereva wa daladala, Novemba 4, mwaka jana, kutamaliza mvutano wa kisheria uliodumu kwa muda sasa kati ya upande wa mashitaka na ule wa utetezi.
Hati hiyo iliyopelekwa Mahakama Kuu inaeleza kwamba, Ditopile alitenda kosa hilo majira ya saa 1:40 usiku, eneo la Lugalo jijini Dar es Salaam kwa kumuua Hassan Mbonde.
Hata hivyo, kuanza kusikilizwa kwa kesi hiyo Mahakama Kuu, kutategemea kukamilika kwa uendeshaji wa shauri hilo, ambalo jana lilitajwa tena katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Lyimo aliwaeleza waandishi wa habari jana kuwa, tarehe ya kuanza kusikilizwa katika mahakama hiyo ya juu haijapangwa kwa kuwa waendesha mashitaka wa kesi ya awali iliyopo Kisutu, hawajafunga ushahidi wao.
Jana, upande wa mashitaka uliiomba Mahakama ya Kisutu tarehe ya kutwaja kwa kesi hiyo kutokana na kutokuwapo kwa maelekezo yoyote kutoka kwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP).
Hayo yalielezwa na Mrakibu Mwandamizi wa Polisi, Germanus Muhume, mbele ya Hakimu Mkuu Mkazi, Michael Luguru.
Mawakili wanaomtetea Ditopile, wao waliiomba mahakama kutoa muda mfupi, hasa baada ya kuwapo kwa taarifa kuwa tayari jalada lilikuwa limeshatoka huko.
Ditopile mwenyewe, jana aliingia mahakamani majira ya saa 4:00 asubuhi, akiwa amevalia shati jeusi lililokuwa na michirizi ya rangi ya maziwa mgongoni, suruali nyeusi, kiatu cheusi huku kichwani akiwa amevaa kofia kubwa aina ya pama kuficha sehemu kubwa ya uso wake.