MWANAFUNZI, Pamela Alfred (22), amejiua kwa kumeza vidonge vingi vya klorokwini kwa kupata daraja la nne katika mtihani wa kidato cha nne, imefahamika.
Pamela ni mkazi wa Modeco, Manispaa ya Morogoro ambaye alihitimu kidato cha nne mwaka jana katika shule ya Adrian Mkoba Mzumbe, wilayani Mvomero, Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai wa Mkoa wa Morogoro, Ahamed Msangi alisema mwanafunzi huyo alijiua Februari 11 mwaka huu baada ya kuangalia matokeo hayo.
Alisema kuwa mwanafunzi baada ya kuona amepata daraja la nne ya pointi 26, alisikitika na kuchukua uamuzi wa kujiua kwa kunywa vidonge hivyo.
Kwa mujibu wa Msangi, baada ya wazazi wake kubaini kuwa amemeza vidogo hivyo walimkimbiza katika Hospitali ya Shaloom, Mazimbu lakini alifariki dunia muda mfupi baada ya kufikishwa hospitalini hapo. Wakati huo huo, Msafiri Kipea (44), mkazi wa Kijiji cha Mvomero, amefariki dunia baada ya kuchomwa na kitu chenye ncha kali katika paji la uso na rafiki yake kutokana na ugomvi wakiwa kwenye ulevi.