MBUNGE wa Mkuranga, Adam Malima (CCM) amesema kwa sasa hana haraka ya kukutanishwa na Mwenyekiti wa IPP, Reginald Mengi na badala yake atakachofanya ni kupitia upya uamuzi wa Spika, Samuel Sitta na kuutafakari.
Akizungumza na gazeti hili jana, Malima alisema kukutanishwa na Mengi siyo kipaumbele chake, ila atahakikisha anasoma tena na tena uamuzi wa Sitta aweze kujiridhisha. “Nataka nipitie tena upya uamuzi ule…nitaupitia mara 20 nitafakari halafu nitasema,”alisema Malima. Malima alisema akiupitia uamuzi huo atagundua Sitta alichomaanisha kutokana na malalamiko ya Mengi na ya kwake ambayo yote yalipelekwa katika ofisi yake. Alisema kwa sasa akisema hatamtendea haki Spika na hatajitendea haki yeye kutokana na uamuzi mrefu ambao Sitta alitumia muda mwingi kuuandaa.
Alikiri kuwa baada ya Spika kutoa uamuzi huo hajapitia tena kusoma kile kilichoandikwa. Hata hivyo hakueleza sababu ya kuamua kutopitia tena uamuzi huo ambao hitimisho lake ni upatanisho.
Gazeti hili liliwasiliana na Malima baada ya maamuzi ya Spika kuhojiwa na wananchi wengi wakitaka kufahamu mambo kadha wanayoona kama yana upungufu. Wengi wanahoji ushahidi wa kanda zilizotumika katika shauri hilo kama hazikuchezewa na pande zote kutokana na kutofautiana.
Katika suala hilo mtaalamu mmoja wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), aliliambia gazeti hili kuwa licha ya kuwa waliitwa kwenye Tume ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, lakini hawakuhusishwa katika kuhesabu muda wa mikanda iliyowasilishwa kama ushahidi.
Mtaalamu huyo ambaye idara yake inahusika na masuala ya vipindi vinavyorushwa katika vituo vya televisheni, alisema tume yake huwa hairekodi taarifa za habari ila inachovitaka vituo hivyo ni kutunza kumbukumbu za taarifa hizo kwa miezi mitatu.
Katika uamuzi alioutoa mwishoni mwa wiki mjini Dodoma, Spika aliamua kuwasuluhisha Malima na Mengi kama njia nzuri ya kumaliza malalamiko ya watu hao wawili. Sitta alisema atawakutanisha kwa madhumuni ya kukubaliana naye utaratibu muafaka utakaojenga suluhu endelevu baina yao na kuepuka hatari ya suala hilo kushamirisha makundi yaliyochomoza ambayo yameonekana kuibua masuala ya udini, rangi na tofauti za vipato katika jamii.