Na Ramadhan Semtawa
NCHI za Afrika Mashariki zimetakiwa kuimarisha miundombinu ya barabara, ili kuharakisha maendeleo ya nchi hizo.
Wito huo umetolewa kutokana na miundombinu katika baadhi ya maeneo ya nchi hizo hasa za vijijini kuwa katika hali mbaya.
Hayo yalielezwa jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Kutengeneza Matairi ya Yana, Erick Kimani, wakati wa uzinduzi wa matairi mapya na kuongeza kwamba miundombinu bora ndiyo ufumbuzi wa ukuaji wa uchumi.
Kimani alisema hivi sasa nchi za Afrika Mashariki zinazungumzia kuwa kitu kimoja, hivyo ni vema zikaangalia jinsi ya kuunganisha miundombinu bora.
Alisema kuna maeneo ya vijijini ambako kunafanyika shughuli za kilimo, lakini bado miundombinu haiko katika hali nzuri.
"Miundombinu hasa barabara nzuri ni jambo la muhimu kwa nchi zetu, matatizo ya Kenya na Uganda hayatofautiani sana na Tanzania, hivyo ni vema tukatilia mkazo suala hilo," alisema Kimani.
Kimani alisema kampuni yake itaendelea kutengeneza bidhaa zinazokidhi hali halisi ya miundombinu ya barabara iliyopo katika nchi ambazo imewekeza.