Na Mussa Juma, Arusha
UBALOZI wa Ufaransa nchini, umefungua kesi dhidi ya Chama cha Wachimbaji Wadogo wa Madini Mkoa wa Arusha (Arema) na Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi nchini (Tucta), ukidai kurejeshewa kompyuta na vifaa vingine vyenye thamani ya dola za Marekani 7,725,000, ambavyo ilivitoa kama mradi kwa chama hicho.
Kesi hiyo ambayo ilitajwa Februari 8, mwaka huu katika Baraza la Nyumba, mbele ya Mwenyekiti wake Hakimu, John Mgetta, Ubalozi huo unadai kompyuta hizo ambazo kwa zaidi ya mwaka sasa zimezuiliwa na kampuni ya udalali ya Mahakama ya Majembe baada ya Arema kushindwa kulipa kodi katika jengo la Tucta.
Katika Kesi hiyo, ubalozi huo unawakilishwa na wakili Elvalson Maro, wakati Arema inawakilishwa na mwenyekiti wake, Hamis Lyoba na Tucta inawakilishwa na Katibu wa Kamati ya Usimamizi wa Jengo lao mkoani hapa, Ernest Kangwa.
Kabla ya Ubalozi huo kuingilia kati, Tucta ilishinda kesi ya kudai kodi ya pango dhidi ya Arena ambao walishindwa kulipia malimbikizo ya kodi kiasi cha Sh630,000, hivyo kampuni ya Majembe kuamuriwa na mahakama kukamata mali zote za chama hicho zikiwemo kompyuta hizo.
Ubalozi wa Ufaransa ulitoa kompyuta hizo kwa mradi wa kusaidia wachimbaji wadogo ujulikanao kama Aden Project, ili kuwasaidia kutafutia masoko pia zingetumika kuendeshea mradi wa Internet, ili mradi ujiendeshe kwa faida.
Kesi hiyo imepangwa kundelea Februari 13 na 20 katika baraza hilo la nyumba mkoa wa Arusha.
Kufunguliwa kwa kesi hiyo pia kumechangiwa na mgogoro unaoendelea kufukuta ndani ya Arena baina yao huku baadhi ya viongozi wakituhumiwa kutumia mradi huo kwa manufaa yao na kutaka mradi huo uhamishie ofisi zake Mererani mkoani Manyara.
Hii ni kesi ya kwanza katika siku za hivi karibuni kwa ubalozi kwenda mahakani kudai kurejeshewa msaada walioutoa kwa taasisi hapa nchini, kutokana na kushindwa kutumika.