Na Jimmy Mengele, Morogoro
UGONJWA wa homa ya bonde la ufa umeingia katika Wilaya ya Kilosa,mkoani Morogoro.
Taarifa hiyo ilitolewa na Afisa Kilimo na Mifugo wa Wilaya ya Kilosa, Remtulah Naftali baada ya kufanyika kwa uchunguzi wa wanyama wafugwao katika eneo hilo.
Akitoa tahadhari kwa wafugaji na walaji nyama wa wilaya hiyo juu ya kuingia kwa ugonjwa huo mara baada ya kumalizika warsha ya kuleta mahusiano baina ya wakulima na wafugaji iliyoandaliwa na Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine (SUA), afisa huyo aliwataka kuacha kula nyama ya aina yoyote mpaka serikali itakapo toa ufafanuzi zaidi.
Naftari alisema baada ya baadhi ya wanyama kupata tatizo la mimba kutoka kila mara, madaktari wa wanyama kutoka Wilaya ya Temeke, Mkoa wa Dar es Salaam walifika wilayani humo kuchunguza sababu hizo ndipo iligundulika kuwa hiyo ni moja ya dalili za ugonjwa homa ya bonde la ufa.
Alisema kutokana na tatizo hilo, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya ilikutana katika kikao cha dharula na kutoa taarifa ya kusitisha mara moja matumizi ya nyama ya ng'ombe, mbuzi, kondoo na nguruwe kwa walaji
Alisema taarifa ya kuingia kwa ugonjwa huo imekuja mwishoni mwa wiki, hivyo wataalam wote wapo katika maeneo ya wafugaji ili kutoa taarifa hiyo ya kuingia kwa ugonjwa huo hatari, ambao mpaka sasa watu wawili wamekufa mkoani Arusha.
Na kutoka Tanga, Burhani Yakub anaripoti kuwa,
watu watano wanashikiliwa na polisi baada ya maafisa wa Idara ya Afya ya Jiji la Tanga kuwanasa wakiuza nyama ya ng'ombe na nguruwe waliochinjwa mitaani katika kipindi hiki cha karantini ya ugonjwa wa boma ya Bonde la Ufa.
Kwa mujibu wa habari zilizopataikana na kuthibitishwa na Mganga Mkuu wa Jiji laTanga,Pili Mtuka ni kuwa watu hao walikamatwa mwishoni mwa wiki katika vitongoji vya Magomeni na Mwakizaro jijini hapa.
Watu walioshuhudia matukio hayo walisema maafisa wa afya kwa kushirikiana na polisi walivamia kitongoji cha Magomeni na kumnasa mfugaji mmoja aliyeamua kumchinja ng'ombe wake wa kisasa na kisha kuuza nyama.
Katika Kitongoji cha Mwakizaro watu wanne walikamatwa wakiwa na nyama ya nguruwe ambayo walikuwa wameitayarisha kwa ajili ya kuiuza, ambapo kabla ya kuanza biashara hiyo walivamiwa na maafisa wa afya waliokuwa wakiendesha msako maalumu Jijini hapa.
Akithibitisha habari hizi, Pili alisema Idara ya Afya imeamua kuendesha msako huo kufuatia Afisa Afya wa Mkoa wa Tanga kutoa maagizo kuwa nyama zote zinzochinjwa mitaani zikamatwe ili kuzuia uwezekano wa maambukizi ya ugonjwa huo.
Tangu kuripotiwa kwa taarifa za mkazi mmoja wa Kijiji cha Mwanyumba aliyekufa wiki iliyopita katika Hospitali ya Bombo akihisiwa kuwa na dalili ugonjwa huo kumewafanya wakazi wa Jiji la Tanga kupunguza kula nyama na kusababisha bidhaa hiyo kutonunuliwa kwenye maduka ya nyama.
Katika tukio kama hilo, mwili wa mkazi wa Kijiji cha Maramba Wilayani Mkinga ,ambaye alikufa wiki iliyopita katika kitongoji cha Magomeni Jijini hapa na kuhifadhiwa chumba cha maiti katika Hospitali ya Bombo amezuiwa kuchukuliwa na ndugu zake kwa ajili ya mazishi, akihofiwa kicho cha kinaweza kuwa kimesababishwa na homa ya Bonde la Ufa.
Kwa mujibu wa habari zilizopatikana katika Hospitali hiyo ni kuwa madaktari wameingiwa hofu baada ya ndugu wa marehemu huyo kushindwa kutoa taarifa sahihi juu ya chanzo cha kifo chake na alikuwa akiishi eneo lilo jirani na sehemu ya makazi ya marehemu Emilia ambaye vipimo vyake vimepelekwa Nairobi kwa uchunguzi.
Kutoka Serengeti, Anthony Mayunga anaripoti kwamba, Mkoa wa Mara, umepiga marufuku uingizaji wa mbuzi, kondoo na ng'ombe kutoka nje ya mkoa, ili kukabiliana na ugonjwa huo.
Amri hiyo imetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Mara, Isidori Shirima, baada ya kuibuka kwa ugonjwa huo mkoani Arusha na kusababisha vifo vya watu wawili.
Amri hiyo ilisomwa jana kwa wataalam wa kilimo na mifugo wilayani hapa, katika mkutano uliofanyika jana kwenye ukumbi wa Isenye na Mshauri wa Mifugo wa Mkoa, Dk Juventus Mzee.
Dk Mzee alisema, utekelezaji wa agizo hilo ulianza Februari 7, mwaka baada ya ugonjwa huo kuripotiwa kuingia nchini.
Dk Mzee alisema taarifa ya mkuu wa mkoa iliyosambazwa kwa wakuu wa wilaya, wakurugenzi wa halmashauri, inasema agizo hilo litadumu hadi hapo, ugonjwa huo utakapomalizika.
Shirima aliwaagiza wakuu wa wilaya za Serengeti na Tarime ambazo zinapakana na maeneo yenye maambukizo ya ugonjwa huo, kusimamia ipasavyo agizo hilo.
Vilevile amepiga marufuku uchomaji wa nyama za ng'ombe, kondoo na mbuzi hadi hapo tishio la ugonjwa huo litakapokwisha na kudhibiti mbu wanaouambukiza.