*Ni Lexus mbili za Sh400 milioni
*Ni kwa ajili ya ofisi ya waziri mkuu
*Yakataliwa hayafai kwa usalama wa viongozi
Na Mwandishi wetu
MIEZI michache tangu serikali itangaze kuanza mchakato wa kupunguza gharama za uendeshaji zinazotokana na wingi wa magari yake ya fahari, imenunua magari mawili ya kifahari aina ya Lexus ambayo gharama yake inakadiriwa kufika Sh400 milioni.
Habari zilizopatikana kutoka serikalini zinaeleza kuwa magari hayo mawili ya kifahari yamenunuliwa na serikali mwaka jana kwa ajili ya ofisi ya waziri mkuu.
Vilevile magari hayo ni miongoni mwa mengine mengi yaliyonunuliwa na kwa kwa ajili ya idara mbalimbali za ofisi hiyo.
Oktoba mwaka jana, aliyekuwa Waziri wa Miundombinu, Basil Mramba, alinukuliwa na gazeti hili akileleza juu ya kuanza hatua za awali za kupunguza manunuzi ya magari ya serikali.
Alisema mpango huo wa serikali ulitolewa kama dokezo katika mwelekeo wa bajeti ya wizara hiyo ya mwaka huu wa fedha kuelekea mwaka 2007.
Ununuzi wa magari hayo mawili ya kifahari aina ya Lexus unaelezwa kuwa ulifanywa na ofisi ya Waziri Mkuu kwa ajili ya matumizi ya Waziri Mkuu.
Hata hivyo, wataalamu wa usalama wa viongozi wakuu wameeleza kutoridhishwa na magari hayo kwa matumizi ya safari za Waziri Mkuu kwa kuwa hayakidhi vigezo vya kiusalama.
Sababu kubwa inayoelezwa na wataalamu hao ni kwamba nafasi baina ya viti vya mbele na vile vya nyuma ni ndogo hivyo kumlazimu kiongozi kushindwa kunyoosha miguu.
Taarifa hizo zilidokeza zaidi kwamba, magari hayo kwa sasa yapo katika yadi za ofisi ya waziri mkuu yakiwa yamekaa.
"Magari yapo, yamepaki ofisi ya waziri mkuu baada ya watu wa usalama kuyakataa yasitumiwe na waziri mkuu," kilifafanua chanzo hicho.
Chanzo hicho kilidokeza zaidi kwamba magari hayo yamenunuliwa nchini Japan na kuingizwa nchini na kampuni moja (jina tunalo).
Alipoulizwa waziri wa miundombinu ambaye kitengo cha magari ya serikali kiko chini ya wizara yake, Andrew Chenge kuhusu magari hayo, alisema hana taarifa kama yapo.
Chenge aliliambia Mwananchi kwa njia ya simu kwamba taarifa hizo huenda zikawa na nia ya kuchafua watu.
"Sina taarifa hizo, maneno mengine yanalenga kuchafua watu, kama una ushahidi niletee," alisema Chenge.
Ikiwa magari hayo yatakubaliwa na kuanza kutumika hii itakuwa ni mara ya kwanza kwa kiongozi wa ngazi ya juu kutumia magari ya fahari aina Lexus tofauti ilivyozoeleka kwa viongozi wa juu nchini kutumia magari aina ya benz.
Uamuzi wa kupunguza matumizi katika nyanja ya ununuzi wa magari ulifikiwa na serikali ili kudhibiti matumizi mabaya ya fedha katika undeshaji wa magari yake.
Gharama za ununuzi wa gari moja aina ya Toyota Land Cruiser Stationwagon VX, ambalo limekwisha lipiwa ushuru wa forodha, kodi ya ongezeko la thamani (VAT) na kondi nyingine kwa mwaka jana zilikuwa wastani wa Sh110milioni.
Kwa utaratibu wa sasa kila mkuu wa kitengo cha serikalini anamiliki gari aina ya 'shangingi'.
Gharama hizo za kununulia shangingi moja ukizilinganisha na ujenzi wa nyumba, zinaweza kujenga wastani wa madarasa 10 ya shule ya msingi au sekondari.
Mpango wa kununuliwa kwa magari hayo ya kifahari umekuwa ukipingwa na Watanzania walio wengi na inapingana na suala halisi ya uchumi wa nchi na umasikini unaowakibili wananchi walio wengi.
Watanzania walio wengi wanaishi katika lindi la umasikini wakiwa na kipato cha chini ya kipato cha dola moja kwa siku.
Tayari baadhi ya nchi za kiafrika zimeaanza kuondokana na matumizi ya magari ya fahari ili kubana matumizi ikiwamo Rwanda.
Utafiti uliofanywa unaoneyesha kuwa serikali nyingi za kiafrika zinatumia fedha nyingi kwa ajili ya ununuzi wa magari ya fahari kwa ajili ya viongozi na watendaji wengine wa serikali kuliko fedha hizo kuwekwa katika shughuli nyingine za maendeleo kama vile sekta ya afya, elimu na barabara.
Nchi nyingi za kiafrika hivi sasa zinalaumiwa na mashirika ya kimataifa likiwamo shirika la kimataifa ya la fedha (IMF) na Benki ya Dunia (WB) kwa kutumia fedha nyingi za bajeti zake katika kununua magari ya fahari kwa watumishi wake,badala ya fedha hizo kuelekezwa katika kuboresha sekta za afya, elimu na miundombinu.
Uchunguzi uliofanywa na mashirika hayo unaonyesha kuwa magari hayo ya kifahari thamani yake inaweza kununulia magari mawili ambayo yanafaa kutumiwa na maafisa wa serikali za kiafrika.