MKUU wa Gereza la Ruanda mkoani hapa, Thobias Otto amekutwa amekufa chumbani kwake huku akiwa ameegemea stuli na mkononi akiwa na dawa ya kutibu ugonjwa wa pumu. Ofisa Mnadhimu Mkuu wa Magereza Mkoa wa Mbeya, Peter Wampandamalishi, alisema kuwa kifo cha Otto kilijulikana jana asubuhi baada ya kuchelewa kuingia ofisini.
Alisema kuwa hadi ilipofika saa mbili asubuhi, Otto alikuwa hajaripoti ofisini, hali iliyomfanya Naibu Mkuu wa Gereza la Ruanda, Fulko Mbunda kutoa taarifa kuwa alikuwa hajafika ofisini, ikizingatiwa kuwa alikuwa na tabia ya kuingia ofisini saa moja asubuhi.
Wampandamalishi alisema kuwa baada ya kupata taarifa hizo, alikwenda nyumbani kwake, akagonga mlango na alipofungua mlango kwa kutumia ufunguo wa akiba alimkuta chumbani kwake ameegemea stuli huku katika mkono wa kulia akiwa ameshika dawa ya pumu aliyoitaja kwa jina la ‘asthmatic’.
Alisema kuwa baada ya kuona hali hiyo daktari aliitwa na baada ya kumkagua, alithibitisha kuwa Kamishna huyo alikuwa amekwisha kufariki dunia. Inakisiwa kuwa alikufa kati ya saa 7 na 8 usiku wa kuamkia jana.
Otto alikuwa na historia ya matatizo ya shinikizo la damu kisukari na pumu, alisema. Otto alihamishiwa mkoani hapa akitokea Makao Makuu ya Magereza Dar es Salaam miezi sita iliyopita.