SERIKALI imesema haitapiga marufuku matumizi ya dawa mpya ya malaria ya ALU, kutokana na madai kuwa ina madhara kwa watumiaji. Badala yake imewataka wananchi kuwa makini na matumizi ya dawa zote kabla ya kupata ushauri wa wataalamu na madaktari.
Akizungumza na HabariLeo kwa njia ya simu jana, Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Aisha Kigoda, alisema kama dawa hiyo ambayo ilizinduliwa hivi karibuni, itapigwa marufuku itakuwa si sahihi na upotoshaji hasa kwa watumiaji. Dk. Kigoda alisema ALU kama zilivyo dawa nyingine kama asprin, panadol na tetracycline, zina mazuri yake na upande mwingine zina madhara yake pamoja na ukweli kwamba bado zinasaidia kuponyesha idadi kubwa ya wagonjwa nchini.
“Hatuwezi kusema dawa hizi zisitumiwe kwani pamoja na kuwapo kwa madhara ambayo yanawatokea baadhi ya watu, bado kuna wengine zinawasaidia. Itakuwa si sahihi kwa upande wao,” alisema Dk. Aisha.
Alisema dawa hupaswa kutolewa na wataalamu ambao wamebobea katika taaluma ya dawa na wao ndiyo humtambua mgonjwa wa kumwandikia dawa hizo na kuwa na uhakika kuwa hazitoweza kumdhuru. Naibu waziri alisema ni kweli dawa hiyo ina matatizo kwa mama anayenyonyesha na mtoto lakini pia inategemea na mama au mtoto mwenyewe, na hilo analitambua daktari pekee.
Alisema tatizo kubwa lililopo ni baadhi ya watu kuwa na tabia ya kununua dawa holela bila kufuata ushauri wa daktari au mtaalamu wa dawa na matokeo yake hudhurika. “Cha msingi ni watu wasinunue dawa ovyo bila kupata maelekezo ya daktari. Wengine hujinunulia na kutumia bila hata wao wenyewe kujijua wanaumwa na ugonjwa gani au hata kuwa na mimba. Sasa kwa nini wasidhurike?” alihoji.
Alisema dawa hiyo inatambuliwa si Tanzania tu bali hata na Shirika la Afya Duniani (WHO) kuwa inatibu vizuri malaria, ila ALU kama zilivyo dawa nyingine haikosi kuwa na madhara kwa baadhi ya watu.