Wananchi wa kijiji cha Nyansha wilayani Kasulu wameulaumu uongozi wa wilaya ya Kasulu kwa kutowapa ushirikiano katika shughuli za maendeleo kijijini mwao.
Lawama hizo wamezitoa mwishoni mwa wiki wakati wa harambee ya kuchangia ujenzi wa shule ya sekondari Nyansha inayojengwa na kijiji vya Nyansha kata ya Mrufyiti.
Wakiongea na Radio Kwizera kwa nyakati tofauti wananchi hao wameelezea kusikitishwa na kitendo cha viongozi wote wa wilaya kutofika katika harambee hiyo licha ya uongozi wa kijiji kutoa myaliko.
Akihutubia katika harambee hiyo mwenyekiti wa serikali ya kijiji cha Nyansha Bw. Bakari Nyamcha amesema kumekuwa na desturi isiyo rasimi ya viongozi ngazi ya Kata na Tarafa kukitelekeza kijiji chao.
Amebainisha kuwa tangu kijiji hicho kianzishe mkakati wa kujenga shule ya sekondari kwa lengo la kupunguza msongamano katika shule yao ya kata ya Mrufyiti uongozi wa wilaya ulijiweka pembeni.
Hata hivyo amesisitiza kuwa licha ya diwani na afisa mtendaji wa kata na viongozi wengine wa halmashauri ya wilaya kualikwa kwenye harambee yao hakuna aliyetoa taarifa za kutohudhulia, na kwamba aliyeomba udhuri ni mkuu wa wilaya pekee.
Kijiji cha Nyansha wilayani Kasulu kimeanza ujenzi wa shule mpya ya sekondari na tayari msingi wa vyumba vitatu vya madarasa umekamilika na hatua za ujenzi wa ukuta zimeanza.