Na Andrew Msechu
CHAMA cha Wanasheria Tanganyika(TLS) kimetuma mjumbe maalum kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linaloendelea mjini Dodoma ili kuliomba Bunge hilo kusitisha kupitisha rasimu ya mabadiliko katika Mkataba wa Afrika Mashariki, hasa kipengele kinachohusiana na uundwaji wa Mahakama ya Rufaa.
Hatua hiyo ya TLS kuwakilisha maombi ya kuzuia kupitishwa kwa rasimu ya mapendekezo hayo ambayo kwa taarifa za awali inatarajiwa kujadiliwa na hatimaye kupitishwa kesho Bungeni mjini Dodoma inafuatia hofu iliyotanda miongoni mwa wanataaluma hao kuwa kwa kufanya hivyo safari kuelekea Shirikisho huru la Afrika Mashariki itakuwa imepata kovu ambalo halitafutika.
Katika mapendekezo hayo, wanasheria hao walisisitiza kuwa endapo marekebisho hayo yatapitishwa katika uvunjwaji wa taratibu zilizowekwa yatawafanya wananchi na wadau kupoteza imani na shirikisho hilo, kwa kuwa kinachoonerkana ndani ni hatari ya udikteta hasa kwa kuwa mapendekezo yaliyopo hasa la kuwaingiza majaji wakuu wa nchi washiriki katika mahakama ya Rufaa.
Mapendekezo hayo yanayoambatana na tamko rasmi la Jumuia hiyo ya wanasheria, yanafuatia maoni ya Jaji Joseph Warioba aliyoyatoa hivi karibuni kuwa utaratibu mabadiliko kufuatia mkataba wa awali katika kufanya mabadiliko haukufuatwa na viongozi wa nchi hizo tatu wamekiuka utaratibu huo kwa ajili ya kufurahisha upande mmoja, suala ambalo gharama yake ni kubwa kwa Jumuia hiyo katika siku zijazo.
Akitoa tamko hilo jijini jana, Mwenyekiti wa Kamati ya Msaada wa Kisheria ya TLS, Alex Mgongolwa alisema ni kweli kifungu cha muhimu cha 150 katika mkataba huo kinachoainisha utaratibu wa mabadiliko hayo, ambacho kinatoa fursa kwa mabadiliko kufanyika katika kipindi cha siku 90 baada ya kushirikisha wadau katika nchi zote shiriki hasa wa kipengele husika.
"Ni dhahiri hili halikufuatwa, inastaajabisha namna kipengele hiki kilivyoharakishwa hasa kwa faida ya kundi linalotoka katika upande mmoja wa Jumuia, utata zaidi unakuja pale Kamati ya Marais ilipokaa kwa siku moja na mchakato mzima kumalizika katika siku 14 tu na kupitisha mabadiliko, huu ni uingiliaji mkubwa wa Uhuru wa Mahakama hii na Uvunjaji wa utawala wa Sheria katika utaratibu mzima," alisema Mgongolwa.
Aliongeza kuwa katika kipindi hiki ambapo nchi hizi zinaelekea katika kuunda jumuia yenye nguvu, ipo haja kwa Tanzania ambayo imekuwa ikisifika kujali na kusimamia utawala wa sheria kwa kipindi kirefu kilichopita kuweka pingamizi katika mabadiliko haya ambayo yanakinzana na dhana hiyo na kulazimisha kulipitisha hilo ni kuharibu mfumo mzima wa utendaji wa Jumuia hiyo kwa siku zijazo.
Hata hivyo, alisema hali hiyo inatia mashaka zaidi kwa kuwa yanaonekana kufanywa kwa shinikizo la upande mmoja ambao awali ulikataa kutambua uwezo wa Mahakama ya Afrika Mashariki iliyopo sasa, ambapo baada ya kushindwa na suala lao kuamuliwa bado walionyesha kutoridhika nayo na kulazimisha kuundwa kwa mahakama hiyo ya Rufaa inayolalamikiwa kutofuata utaratibu.
"Maadam Rais Kikwete ameshasema kuwa yuko tayari kuelemishwa katika hili, sisi tuko tayari kuelimisha, tunaomba Bunge liahirishe hoja hii, wadau wapewe muda kulipitia na kuwasilisha mapendekezo juu ya mfumo huo utakavyokuwa, hakuna hasara ya kusogeza mbele ili kupata mtazamo sahihi, kulilazimisha ni kujitumbukiza katika matatizo makubwa siku zijazo," alisema Mwansheria Ibrahim Bendera.