MBUNGE wa Same Mashariki, Anne Malecela, ameishauri serikali kusimamisha uchimbaji wa madini ya Tanzanite hadi hapo wawekezaji wa ndani watakapokuwa na uwezo wa kuyachimba madini hayo.
“Waziri Mkuu wa Malaysia aliwahi kufunga migodi yake hadi nchi ilipopata uwezo wake wenyewe wa kuyachimba. Tusipofanya hivyo, hao wawekezaji wa nje watakuwa wanayahifadhi hadi hapo yatakapokwisha ndiyo waanze kuyauza tena,” alishauri Mbunge huyo.
Kilango alikuwa akiuliza swali la nyongeza kwa Wizara ya Nishati na madini, lililotokana na swali lake la msingi alilotaka kujua mpango wa serikali katika kujitayarisha kujikomboa kwa kuchimba madini hayo bila kutegemea wawekezaji wa nje.
Akitoa majibu ya nyongeza, Waziri wa Nishati na Madini, Nadhir Karamagi alisema kwamba serikali haiwezi kufunga uzalishaji wa madini hayo wala kufukuza wawekezaji kwa kuwa itajikoseshea mapato.
Hata hivyo alisema serikali inaandaa mazingira bora ya uchimbaji wa kisasa ambao hauna athari kubwa.
Alisema kutokana na maendeleo ya teknolojia, kwa sasa upo uwezekano wa madini kuchimbwa bila kuisha ardhini, hivyo hakuna sababu ya kuhofia ikizingatiwa kwamba serikali ina mikakati madhubuti ya kuwasaidia wachimbaji wa ndani, ili waweze kunufaika na kazi wanayoifanya.
Waziri huyo pia alimhakikishia Mbunge wa Simanjro, Christopher Ole Sendeka ambayo jimbo lake ndilo linalotoa madini ya Tanzanite kwamba serikali itatoa kipaumbele kwa wachimbaji wadogo katika kugawa maeneo mapya ya migodi inayotarajiwa kufunguliwa.
Awali, Naibu Waziri wa Wizara hiyo, William Ngeleja, alisema serikali ina mkakati wa kuziandikisha kampuni za madini kwenye Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), ili kuwawezesha watanzania wenye uwezo kumiliki migodi.
Alisema pia serikali inaandaa utaratibu wa kuwasaidia wachimbaji wadogo kupata mikopo na maarifa mapya katika fani ya uchimbaji, pamoja na kuwahimiza wenye leseni za uchimbaji madini kufanya tafiti kisha kutafuta wabia watakaoziendeleza.