WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Profesa Mark Mwandosya amewashauri Watanzania kukataa misaada ya kompyuta na simu za mitumba ili kuiepusha Tanzania kugeuka dampo la taka za sumu za kielektroniki.
Waziri Mwandosya alisema kuwa nchi zilizoendelea zinakuwa dampo la taka za sumu zitokanazo na vifaa hivyo vya elektroniki jambo linaloweza kuleta balaa kubwa nchini.
“Ushauri wangu ni kwamba zikataeni..., na kwa kweli tunatarajia kuweka utaratibu wa kudhibiti vifaa hivi siku za baadaye,” alisema Mwandosya.
Mwandosya aliyekuwa akijibu hoja za wabunge waliochjangia katika hoja yake ya kulitaka Bunge kuridhia Mkataba wa kuundwa kwa Kituo cha Afrika cha Usimamizi wa taka za sumu na nyinginezo.
Akizungumzia dawa ya DDT yenye mjadala mkali juu ya usalama wa matumizi yake, Mwandosya alisema tani tano za dawa hiyo zitahitajika katika wilaya 25 zenye mlipuko mkubwa wa ugonjwa wa malaria nchini.
Alisema kuwa katika wilaya hizo, DDT itatumika kudhibiti mbu na kwamba kazi hiyo litahitaji usimamizi mkubwa ili kupunguza athari zitokanazo na kemikali hizo.
Kwa mujibu wa Mwandosya, taka zenye sumu zina madhara makubwa kwa binadamu na mazingira na kwamba nyingi kati ya taka hizo zina tabia ya kuchuna vyuma na ngozi ya viumbe hai.
Tabia nyingine ya taka hizo ni kuwaka moto zenyewe katika joto la nyuzi joto 60 , kulipuka na kusababisha madhara makubwa katika muda mfupi na mrefu.
Alisema kuwa kituo hicho kitakachojengwa Afrika kusini kitakuwa na jukumu la kutoa mafunzo, teknlojia, utoaji wa habari na ushauri na kukuza uelewa wa jamii kuhusiana na usimamizi wa taka za sumu na za kawaida.