AFISA mmoja wa Ubalozi wa Tanzania nchini Malawi amepewa adhabu ya kulipa Sh33,887,569, baada kubainika kufanya ubadhilifu wa fedha za serikali.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje, Dk. Cyril Chami, aliliambia Bunge jana, mjini hapa kwamba afisa huyo ambaye alizipata fedha hizo kwa kukiuka taratibu za ununuzi wa umma, atazilipa kupitia makato katika fedha yaze ya pensheni.
Dk Chami alieleza kwamba baada ya kuwepo kwa tuhuma hizo, Mei mwaka jana afisa huyo aliitwa kuhojiwa na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali, ambayo iliahidi kutoa mapendekezo juu ya hatua sahihi za kinidhamu za kuchukuliwa kwa afisa huyo.
Chami alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Gando, Khalifa Suleiman Khalifa, aliyetaka kujua ni katika balozi zipi za nje hali ya ubadhilifu wa fedha ya umma imejitokeza na hatua zipi zimechukuliwa kwa wahusika.
Naibu Waziri huyo alidai ofisi nyingine za ubalozi zilizokumbwa na tuhuma za ubadhilifu wa fedha za umma ni za Rome, Italia ambapo maafisa wanaotuhumiwa kuhusika na ubadhilifu huo wameshafikishwa mahakamani.
Katika swali la nyongeza la Bunge wa Karatu, Dk Wilbrod Slaa, aliitaka serikali kutoa maelezo ya ni kwa namna gani na lini fedha nyingine zaidi ya Sh100 milion zinazodaiwa kufujwa na balozi nyingine zitarejeshwa na endapo serikali iko tayari kuwabana wezi wengine kurejesha fedha walizofuja kama ilivyofanyika kwa ubalozi wa Malawi.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri Chami alisema wizara hiyo haijishughulishi na kukamata wezi, isipokuwa huwashughulikia wanaokiuka taratibu za ununuzi. Hata hivyo alisema bado serikali inaendelea kufuatilia hali ya mambo katika balozi nyingine.