Na Muhibu Said
VYAMA vya upinzani vimeanza mbio za kuwania ubunge katika uchaguzi Mdogo wa Jimbo la Tunduru kuziba nafasi iliyoachwa wazi na aliyekuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu marehemu Juma Akukweti.
Wakati vyama vyama vya Chadema na CUF vinakusudia kusimamisha wagombe, Tanzania Labour Party (TLP) kimeamua kumuunga mkono mgombea wa CUF, kwa madai kuwa ndiye anayekubalika.
Mwenyekiti wa TLP, Augustine Mrema, amevishauri vyama vingine vya upinzani kuutumia uchaguzi huo kujenga ushirikiano baina yao kwa kumuunga mkono mgombea wa CUF.
Akizungumza na Mwananchi jijini Dar es Salaam jana, Mrema alisema anashauri suala hilo ili kuepuka kurejea makosa yaliyofanywa na chama chake, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) na NCCR-Mageuzi katika Jimbo la Vunjo, mkoani Kilimanjaro, katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka juzi.
Alisema katika uchaguzi huo, vyama hivyo vilikataa kushirikiana, badala yake kila kimoja kikasimamisha mgombea, uamuzi ambao ulitoa mwanya kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuchukua jimbo hilo.
"Sitaki kuinufaisha CCM, kama kweli wapinzani tunataka tushinde, tuanze kushirikiana, kupendana na kuwa wamoja katika uchaguzi wa Tunduru," alisema Mrema.
Mgombea wa CUF aliyewania kiti hicho na kuangushwa na Akukweti katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka juzi jimboni humo, ni Naibu Mkurugenzi wa Blue Guards ambaye pia ni Naibu Katibu wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Taifa ya chama hicho, Mazee Rajab.
Kaimu Mkurugenzi wa Haki za Binadamu na Mahusiano na Umma wa CUF, Mbarallah Maharagande, aliliambia Mwananchi jana kuwa chama chake kinatarajia kumpitisha tena Rajab kuwania kiti hicho katika jimbo hilo.
Hata hivyo, wakati Mrema akishauri hivyo, Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Shaibu Akwilombe, aliliambia Mwananchi jana kuwa katika uchaguzi huo, chama chake kitasimamisha mgombea.
Akwilombe alisema tayari yeye mwenyewe amekwishapitishwa na Chadema Wilaya ya Tunduru na kwamba anachokisubiri hivi sasa ni kupitishwa na vikao vya ngazi za juu vya chama.
Tayari Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imekwisha kutangaza tarehe ya uchaguzi jimboni humo ambao unatarajiwa kufanyika Machi 18, mwaka huu.
Kwa mujibu wa NEC, Februari 20, imepangwa kuwa siku ya uteuzi wa wagombea na kampeni za uchaguzi huo zimepangwa kuanza rasmi Februari 21 hadi Machi 17, mwaka huu.