Timu za netiboli za Zanzibar mwaka huu hazikusajili wachezaji kutoka Tanzania Bara kwa ajili ya ligi kuu itakayoanza Juni kwenye uwanja wa Gymkhana, imeelezwa.
Katibu Mtendaji wa Chama cha Netiboli cha Zanzibar, CHANEZA, Sharrifa Khamis ’Sherry’ alisema kwa njia ya simu mwishoni mwa wiki kuwa baada ya kupitia fomu za usajili, imebainika kuwa timu zote zimesajili wachezaji kutoka visiwani tu.
Sherry alisema tofauti na miaka ya nyuma ambapo wachezaji wengi wa Bara walikuwa wakikimbilia Zanzibar kusajiliwa na timu za huko, mwaka huu hakuna timu iliyochukua wachezaji kutoka upande wa pili wa Muungano.
’’Haieleweki kwa nini mwaka huu hakuna, ila ni mara ya kwanza kwa timu zetu kukosa wachezaji wa Bara,’’ alisema Sherry na kuongeza \”lakini ninaona sasa wameanza kuona umuhimu wa wachezaji wa visiwani kuwa nao wana uwezo mkubwa wa kucheza netiboli.’’
Timu za visiwani kwa wanawake ni mabingwa watetezi wa ligi kuu JKU, Polisi, Nyuki, Bandari, Mafunzo, Zimamoto, Chipukizi na Afya wakati za wanaume ni JKU, Msambweni, Nyuki na Polisi.
SOURCE: Lete Raha