Na Mwandishi Wetu
NAIBU Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Cyril Chami ameorodhesha bungeni changamoto zinazoukabili Umoja wa Afrika (AU) kuhusu msimamo wa kuhakikisha Kisiwa Mayote kinarudi katika Dola ya Comoro.
Dk Chami alizitaja changamoto hizo jana wakati akijibu swali la msingi kuwa ni pamoja na raia wake kupiga kura mara mbili na kuamua kubaki chini ya ukoloni wa Ufaransa.
Viongozi wa ndani wa kisiwa hicho, kupendelea zaidi kuwa chini ya Ufaransa kuliko kujiunga na wenzao wa Muungano wa Comoro.
Ufaransa ambayo inapendelea kukitawala kisiwa hicho kuwa taifa lenye kura ya turufu katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa hivyo kuwa na uwezo wa kupinga pendekezo lolote linalokusudia kukiweka chini ya utawala wa Comoro.
Katika swali la nyongeza, Mbunge wa Kwela, Chrisant Mzindakaya alitaka kujua iwapo Umoja wa Afrika hauna sauti kuhusu nchi za Afrika zinazoendelea kutawaliwa na ukoloni ,kikiwamo kisiwa hicho, na iwapo ni haki kwa Ufaransa kuendelea kukitawala.
Dk Chami alisema umoja huo, utasaidia wanaohitaji msaada wao na unaheshimu utashi wa nchi husika kikiwamo kisiwa hicho ambacho kimeamua kuendelea kuwa chini ya ukoloni wa Ufaransa.