MASHINDANO ya karate kwa shule za msingi, sekondari na vyuo yanatarajiwa kufanyika Aprili mwaka huu jijini Dar es Salaam.
Akizungumza jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki, Rais wa Chama cha Karate Tanzania (TASHOKA), Sensei Willy Ringo, alisema mashindano hayo yatawashirikisha wanafunzi watakaopenda kutoka shule za msingi, sekondari na vyuo kutoka jijini Dar es Salaam, lengo likiwa ni kuelekea kuwaunganisha na wenzao wa Kanda ya Tano Afrika.
Rais huyo aliwataka wanafunzi watakaopenda kushiriki mashindano hayo kuonana na uongozi wa TASHOKA ili kupata maelekezo zaidi.
Ringo pia alitoa wito kwa walimu watakaokuwa wakiwanoa washiriki hao, kufanya maandalizi ya kutosha kimazoezi ili kuwapa mwamko wa kuupenda mchezo huo.
“Hata walimu ambao watakuwa na jukumu la kuwafundisha wanafunzi hawa, itabidi nao tuonane kwa lengo la kupanga mikakati ya kutosha kuhusiana na maandalizi kamili ya mashindano hayo na mbinu za mazoezi zinazopaswa kufuatwa kabla ya kufanyika kwa mashindano,” alisema.