Na Mwandishi Wetu, Morogoro
MKULIMA Amos Bwayonga (36), wa Ruaha, wilayani Kilosa anadaiwa kutekwa nyara na wafugaji wa jamii ya kimasai toka Januari kumi, mwaka huu na hajaonekana wala haijulikani kama yuko hai.
Wakizungumza na waandishi wa habari mjini hapa, ndugu wa mateka huyo, Timotheo Lucas na Josephat Majebwe, walisema hawana matumaini ya kumpata ndugu yao akiwa hai, kutokana na jitihadi walizozifanya kwa kushirikiana na polisi na
wananchi wa eneo hilo kushindwa.
Lucas alifahamisha kuwa tukio hilo lilitokea katika kijiji cha Kisisi, Kata ya Malolo, Tarafa ya Mikuni, wilayani Kilosa Januari 10, mwaka huu majira ya saa 11.00 jioni akiwa shambani na mwenzake mmoja, ambapo wafugaji hao baada ya kufika katika eneo hilo wakamwita Bwayonga, kisha waliondoka naye lakini hakureja na mpaka sasa hajulikani alipo.
Juhudi za kumsaka mtu huyo zilifanyika mpaka usiku wa manane kwa kushirikiana na polisi wa Kituo cha Ruaha, ambapo walifanikiwa kuwatia mbaroni watu wawili kati ya watatu wanaotuhumiwa kushiriki katika tukio hilo, ambao baada ya kuhojiwa walikiri kuondoka na mtu huyo bila kubainisha alipo.
Lucas alidai kuwa baada ya upelelezi wa polisi kufanyika, ilibainika kuwa mtuhumiwa wa tatu anayedaiwa kushiriki katika tukio hilo, ambaye alifanikiwa kutoroka katika mtego wa polisi, ndiye aliyeondoka na mtu huyo hadi kwenda
Kijiji cha Madaganya, Rujewa, mkoani Mbeya.
Polisi katika kituo cha Mikumi ambako kesi hiyo iliripotiwa walitoa hati ya kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo, yenye kumbukumbu MK/IR/35/2007 ambapo Januari 15, Lucas alikwenda Rudewa, akatoa taarifa katika Kituo cha Polisi Chimala na Januari 16 alipewa mgambo mmoja ili kwenda kumkamata mtuhumiwa na kufanikiwa kumtia mbaroni, lakini alifanikiwa kuwatoroka wakiwa njiani kumpeleka kituoni.