Na Mussa Juma, Arusha
MAPATO ya Mamlaka ya Hifadhi za Taifa (TANAPA) yamefikia Sh45.6bilioni kutoka mwaka 1995/6 hadi 2005/6.
Takwimu za kuongeza kwa mapato ya mamlaka hiyo kutoka Shilingi 5.9 bilioni na kufikia Shilingi 45.6 bilioni zimetolewa na Mkurugenzi Mkuu wa TANAPA, Gerard Bigurube wakati akisoma taarifa za kwa Kamati ya Bunge ya Maliasili na Mazingira.
Bigurube alisema kuwa, mapato hayo yanarajiwa kuongezeka hadi kufikia shilingi 60 bilioni kwa mwaka 2006/7 mapato ya mamlaka hiyo, ikiwa mikakati iliyowekwa na mamlaka hiyo itafikiwa.
Mikakati hiyo ni pamoja na kuboresha utendaji wa mamlaka, kupanua wigo wa utalii, kundeleza utalii wa ndani, kutoa mafunzo kwa watendaji na wadau wengine juu ya uhifadhi wa utalii na ufuatiliaji wa mabadiliko ya mazingira ndani na nje ya hifadhi.
Mwaka 2000/1, mamlaka hiyo ilikusanya shilingi 16.4 bilioni wakati lengo lilikuwa ni kukusanya shilingi 15.2 bilioni.
Mwaka 2001/2 shilingi 17.8 bn (14.7 bn), mwaka 2002/3 shilingi 23.1 bn (19.3 bn), mwaka 2003/4 shilingi 25.6 bn na (22.8 bn), 2004/5 shilingi 33.2 bn (30.7 bn) wakati mwaka 2005/6 shilingi 45.6 bn (37.9 bn).
Hata hivyo mamlaka hiyo inakabiliwa na matatizo baadhi yakiwa ni mabadiliko ya kiikolojia kwenye hifadhi hali inayosababisha uharibifu wa mazingira,mazingira magumu kwa wafanyakazi ambao wengi wao wanaishi porini na kuwepo na baadhi ya watumishi ambao ni waaminifu ambao hata hivyo wamekuwa wakishughulikiwa.
Akizungumza baada ya kupokea taarifa hiyo, Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Hassan Rajab Khatibu Mbunge wa Aman Zanzibar, alipongeza TANAPA kwa utendaji mzuri hivyo kupewa hati ya bora ya mahesabu kwa miaka 15 mfululizo.
Khatibu alisema jitihada za mamlaka hiyo ni kubwa katika kuimarisha utalii na kutunza hifadhi za taifa, hivyo zinapaswa kupongezwa na Watanzania wote na kuungwa mkono