Habari Tanzania - http://www.habaritanzania.com
Moro United watakiwa kukaza buti waitwe Stars
http://www.habaritanzania.com/articles/27/1/Moro-United-watakiwa-kukaza-buti-waitwe-Stars
By Habari Tanzania
Published on 05/14/2006
 
Wachezaji wa timu ya Moro United ya Morogoro wametakiwa kujituma zaidi kwenye mazoezi na uwanjani na hatimaye kuongeza kiwango cha uchezaji ili wachaguliwe kwa wingi katika timu ya taifa, Taifa Stars.

Wachezaji wa timu ya Moro United ya Morogoro wametakiwa kujituma zaidi kwenye mazoezi na uwanjani na hatimaye kuongeza kiwango cha uchezaji ili wachaguliwe kwa wingi katika timu ya taifa, Taifa Stars.
 
Moro United ndiyo timu pekee nchini iliyobaki kwenye michuano ya klabu ya Afrika lakini ina wachezaji wawili tu katika kikosi cha Taifa Stars kilichofanya kambi ya wiki moja mapema mwezi huu ambao ni mlinda mlango Farouk Ramadhani na mshambuliaji Nsa Job.
 
Ushauri huo kwa wachezaji wa Moro United umetolewa na mshauri wa ufundi wa timu hiyo Abdallah Kibadeni ambaye alisema jijini katikati ya wiki kuwa wachezaji wake wanatakiwa kuwa na usongo wa kutafuta nafasi za kuitwa Stars kwa kuanzia na michuano ya klabu bingwa ya Afrika Mashariki na kati, Kombe la Kagame na baadaye ligi kuu itakayoanza tena Mei 31.
 
’’Sasa hii ni changamoto kwa wachezaji kufanya vyema ili wakaongeze idadi ya wachezaji waliopo Stars,’’ alisema Kibadeni.
 
Moro United ni miongoni mwa timu nane bora nchini kwa miaka kadhaa sasa na uchache wa wachezaji kwenye timu ya taifa unamuudhi Kibadeni. Moro imeondokewa na wachezaji nyota saba hatahivyo msimu huu.
 
Timu zinazoongoza kwa kuwa na wachezaji wengi Stars ni Yanga na Mtibwa Sugar ambazo zimetoa wachezaji saba.
Wachezaji wa Yanga kwenye timu ya taifa ambao wawili kati yao walikuwa Moro United msimu uliopita ni Ivo Mapunda na Shadrack Nsajigwa, Nadir Haroub ’Canavaro’, Hamis Yussuf, Said Maulid, Mohamed Banka na Gulla Joshua.
 
Wachezaji wa Mtibwa Sugar kwenye kikosi cha Stars ni Mecky Mexime, Amir Maftaha, Salum Swedi, Said Mkopi, Abdi Kassim, Nizar Khalifan na Abdallah Juma.
 
Simba ya Dar es Salaam ina wachezaji wanne Stars ambao wawili kati yao walikuwa Moro United misimu mitatu nyuma ambao ni Juma Kaseja na Ulimboka Mwakingwe, na Mussa Hassan ’Mgosi’ na Athuman Idd.
 
SOURCE: Lete Raha