BAADHI ya watendaji katika Manispaa ya Temeke, wamejiingiza katika kitendawili kigumu baada ya kushidwa kuwasilisha nyaraka maalumu za gari la zimamoto (Manufactural Warrant) katika Wizara ya Miundombinu ili kupata usajili kama ilivyoelekezwa na wizara.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili na kuthibitishwa na vyanzo vyetu katika Wizara ya Miundombinu, umebaini kuwa watendaji wa manispaa hiyo wameshindwa kuwasilisha nyaraka hizo na inaaminika kuwa hazipo.
Hata hivyo, inaelekea kuwa gari hili si jipya kama ilivyodaiwa na manispaa hiyo kwani imeshindwa kuwasilisha nyaraka hizo. Iwapo itathibitika kuwa gari hili si jipya, ni dhahiri kuwa baadhi ya watumishi wa manispaa hiyo watatakiwa kutoa maelezo ni kwa nini walidanganya kuwa gari hilo ni jipya.
Aidha, watatakiwa watoe maelezo ya kina kwa nini wametumia fedha nyingi kununua gari lililotumika, fedha ambazo zingetosha kununulia gari jipya.
Habari zilizopatikana zinaeleza kuwa siku moja baada ya gazeti hili kuripoti kwa mara ya kwanza sakata hilo, watendaji kutoka manispaa hiyo waliwasilisha nyaraka za mkataba wa ununuzi wa gari, nyaraka ambazo hakizuhitajika wizarani.
Nyaraka hizo za mkataba wa ununuzi zenye kurasa mbili, ziliwasilishwa na watendaji wa manispaa wakiwamo Mwanasheria na Ofisa Usafirishaji siku ya Januari 12.
Hata hivyo, maofisa wa wizara walizikataa nyaraka hizo kwa kuwa si ambazo wanazihitaji ili kusajili gari hilo.
“Nyaraka hizo za mkataba wa ununuzi hazitoshi na wala haziwezi kuthibitisha kuwa gari ni jipya, nashindwa kufahamu tatizo liko wapi kwani ‘Manufactural Warrant’ ni nyaraka ambayo huwa inaambatanishwa na nyaraka nyingine.
“Na kama kweli ni jipya ina maana wanashindwa kuwasiliana na kampuni husika ili kuipata nyaraka hiyo? Ninaamini kuwa kama wangefanya hivyo wangeletewa nyaraka hiyo haraka, lakini kwa muda ambao wamekuwa wakiitafuta, inatia wasiwasi kwani si manispaa ya kwanza kutuyumbisha na magari yenye utata,” kilieleza chanzo hicho.