WAFANYABIASHARA wanaosafirisha mbao kutoka Mafinga, mkoani Iringa kuja Dar es Salaam, wamemtuhumu ofisa misitu mkoani humo kwa kuweka mawakala wa kuwauzia vibali vya usafirishaji kinyume cha sheria.
Ofisa mistu huyo aliyefahamika kwa jina moja la Mchome, anadaiwa kuwa amekuwa akiwanyima wafanyabiashara hao vibali vya kusafirisha mbao na magogo, vinavyojulikana kama Transit Pass For Forest Produce, ambacho kwa kawaida hutolewa bure na ofisi yake ili kuwapa uhalali wa kusafirisha mzigo.
Wafanyabiashara hao wanamtuhumu ofisa misitu huyo kuwa amewapa uwakala vijana ambao anawapatia vibali hivyo kutoka Iringa mjini na kwenda kuwauzia huko Mafinga kinyume na utaratibu wa awali ambapo ofisi hiyo ilikuwa ikivitoa bure.
Kwa mujibu wa maelezo yao, wao hawapaswi kulipia vibali hivyo kwani wapasuaji mbao wanalipa ushuru wote na wao wanapaswa kulipa baada ya kufika Dar es Salaam.
Akizungumza katika ofisi ya Tanzania Daima, mmoja wa wafanyabiashara hao, Thomas Msigwa, ambaye ameifanya biashara hiyo kwa zaidi ya miaka sita, alisema awali kibali hicho kilikuwa kinapatikana kwa urahisi katika ofisi ya mkuu huyo lakini kwa sasa kila wakifika katika ofisini iliyopo Iringa mjini wanaambiwa kuwa vibali havipo.
Hata hivyo, alidai kuwa wakienda Mafinga, wanakuta vinauzwa na vijana mitaani kwa sh 15,000.
“Tunashangaa sana kuambiwa hakuna vibali huku vinauzwa mitaani, tena vimegongwa mhuri wa serikali na saini ya Mchome, halafu yeye anakwenda kutusubiria kwenye geti la Ndyaka, unamkuta anajifanya anakagua vibali, ukimuonyesha wala hakuulizi umetoa wapi,” alidai Msigwa.
Ofisa mistu huyo anatuhumiwa pia kuwa anatumia vibaya madaraka kwa kutumia kitabu cha Halmashauri ya Kilolo kwa ajili ya kukusanya ushuru kinyume, wakati kazi ya kukusanya ushuru ni ya Mkurugenzi wa Halmashauri.
“Ona hiki kibali alichonikatia ushuru wa sh 50,000 wakati kinaonyesha ni cha Kilolo lakini yeye alikatia katika geti la Ndyaka ambalo lipo Iringa,” aliongeza.
Tanzania Daima inazo nakala mbili za vibali ambazo wafanyabiashara hao wanadai kuwa zimetolewa na ofisa misitu huyo kwa njia ambazo si halali.
Alipotafutwa atoe ufafanuzi, Mchome aliwalaumu wafanyabiashara hao kuwa wao ndio hujikusanya pamoja na kutuma mawakala wanaokwenda kuwachukulia vibali.
Hata hivyo, alikiri kuwa wapo mawakala wawili waliopewa kazi ya kukatisha ushuru na kutoa vibali hivyo bure.