KATIKA kile kitakachokuja kupigiwa upatu baadaye, kuwa ni juhudi za serikali kupambana na ufisadi, serikali jana ilimfikisha mahakamani, aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Costa Ricky Mahalu na wenzake wawili, kujibu tuhuma za kuhujumu uchumi.
Iwapo atapatikana na hatia, Balozi Mahalu atakabiliwa na kifungo kisichozidi miaka 15 jela kwa mujibu wa sheria zilizopo.
Pamoja na Balozi Mahalu, wengine waliopandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, ni Steward Migwano, aliyekuwa Mhasibu na Grace Martin, aliyekuwa ofisa utawala ubalozini Italia.
Watuhumiwa hao walifikishwa mbele ya Hakimu Mkuu Mfawidhi, Sivangilwa Mwangesi, kujibu mashitaka matano katika kesi ya uhujumu uchumi namba moja ya mwaka huu.
Ilidaiwa na Mwendesha Mashitaka wa Taasisi ya Kuzuia Rushwa nchini (TAKURU), Joseph Ole, kuwa, watuhumiwa hao na wengine ambao hawakuwapo mahakamani, walikula njama ili kuiibia serikali.
Katika shitaka la pili, wanadaiwa kuwa, Septemba 23, mwaka 2002 katika Jiji la Roma nchini Italia, wakiwa waajiriwa wa Serikali ya Tanzania, waliandaa hati ya malipo yenye namba D2/9 ya siku hiyo, kwa maelezo ya uongo kuwa, hayo ni malipo ya ununuzi wa jengo lenye thamani ya Euro 3,098,741.58 huku wakijua kuwa si kweli.
Shitaka la tatu linalowakabili, ni kutumia hati ya kupotosha kwa nia ya kujipatia fedha. Inadaiwa kuwa, Oktoba mosi, 2002, watuhumiwa hao walitumia mkataba wa mauzo wenye maelezo ya uongo, kwamba walinunua jengo lenye thamani ya Euro 3,098,741.58 kwa nia ya kuipotosha serikali.
Wanadiwa kwamba, kwa nia ovu, waliwasilisha mkataba wa uongo kwa Serikali ya Tanzania kuwa, raia wa Italia amepokea jumla ya Euro 3,098,741.58 kama mauzo ya jengo kwa ajili ya Ubalozi wa Tanzania nchini humo.
Pamoja na mashitaka hayo, wakiwa watumishi wa serikali, wanadaiwa kuiba Euro 2,065,827.60 mali ya Serikali ya Tanzania na kulisababisha hasara taifa.
Watuhumiwa wote walikana makosa hayo na kupatiwa dhamana kwa masharti ya kuwa na wadhamini wawili wa kuaminika watakaosaini mkataba wa sh milioni tano kila mmoja.
Aidha, watuhumiwa hao wametakiwa kuwasilisha hati zao za kusafiria na kupigwa marufuku kutoka nje ya jiji bila kibali cha mahakama. Hakimu Mwangesi, aliahirisha kesi hiyo hadi Februari 20, mwaka huu itakapotajwa tena kwa kuwa upelelezi haujakamilika.
Kabla ya kupandishwa kizimbani, Balozi Mahalu, aliyevalia suti nyeusi, alionekana kukwepa kamera za waandishi wa habari, kwa kujificha ndani ya gari namba T 385 ALK, Toyota Land Cruiser, lililokuwa mbele ya Mahakama ya Watoto.
Watuhumiwa wote walifikishwa mahakamani hapo chini ya uangalizi wa askari wa PCB saa 4:40 asubuhi.
Kesi hiyo imekuja wakati serikali ipo katika hatua za mwisho, kukamilisha muswada wa sheria ya rushwa. Muswada huo mpya, unaotarajia kujadiliwa katika vikao viwili vya Bunge (kikao cha Januari na Aprili), umeongezwa makosa ya rushwa.
Makosa yaliyoongezwa katika sheria hiyo, inayopendekeza muundo mpya wa TAKURU, ni rushwa katika mikataba, manunuzi au ugavi, minada na rushwa inayofanywa na watumishi wa sekta binafsi badala ya watumishi wa umma pekee, kama rushwa katika ajira na rushwa ya ngono