Na James Magai
MIEZI michache tangu kuondolewa katika mitaa na maeneo yasiyoruhusiwa kwa shughuli za biashara, wafanyabiashara ndogo ndogo (wamachinga) wamerudi rasmi katika baadhi ya maeneo hayo, huku baadhi yao wakidai kuwa zile zilikuwa nguvu za soda tu.
Ingawa katika siku za mwanzoni baada ya kuondolewa na kupelekwa katika maeneo waliyotengewa , baadhi yao waliendelea na shughuli zao katika maeneo hayo kwa kujificha ficha, sasa wameamua kuendesha shughuli hizo wazi wazi kuanzia majira ya jioni hadi kwenye muda wa saa 4:00 hivi za usiku.
Wakizungumza na mwandishi wa habari hii baadhi ya wamachinga hao walisema wameamua kurejea kwa sababu walikohamishiwa hakuna biashara kwa vile maeneo hayo yako mbali na wateja na kwamba sehemu nyingine hakuna hata usafiri.
"Unajua biashara ni watu, sasa kule walikotupeleka hakuna watu, wateja hawafiki kabisa kwa sababu kwanza ni mafichoni na hakuna hata usafiri wa rahisi wa kuwafikisha huko. Kwa ujumla hakuna biashara huko unaweza kukaa hata wiki nzima hujauza kitu.
“Mimi nilikuwa pale Redio Tanzania. Nilikaa kwa juma zima nikauza siku mbili tu tena kifaa kimoja kimoja kila siku wakati huo huo unatakiwa kula, usafiri, pesa ya kutunzia mizigo, kodi ya nyumba na mambo mengine. Wengine wana familia, sasa unadhani tutawezaje kumudu wakati biashara hakuna? alihoji Hashimu Athumani anayefanya biashara ya kuuza mabegi madogo ya wanafunzi katika eneo la Buguruni Sokoni.
Alisema kutokana na hali ngumu kibiashara katika maeneo waliyotengewa kuna wengine wamekula mitaji na kushindwa kuendelea na biashara na kwamba, wengine wameamua kuacha na kwenda kuangalia hali mikoani.
Pamoja na ugumu wa biashara katika maeneo hayo wamachinga hao walilalamikia utaratibu uliotumika kuwapatia maeneo hayo na kusema kwamba mwenye nguvu tu kifedha ndiye aliyeweza kupata eneo.
Machinga mwingine ambaye hakutaka kujitambulisha jina lake alisema, wameamua kurudi na kuendesha biashara usiku kwa kuwa muda huo saa za kazi za serikali huwa zimekwisha na kwamba hawaoni kama kutakuwa na usumbufu wowote kwa watu wengine.
“Hata hivyo suala la kutuondoa katika maeneo haya limekuwa ni la jadi kwani kila Mkuu wa Mkoa anayekuja amekuwa akilipigia kelele hivyo hivyo lakini baadaye linatulia .Hata sasa limeanza kupoa,” alisema mmachinga huyo.