Na Midraji Ibrahim
WAZIRI wa Habari, Utamaduni na Michezo, Muhammed Seif Khatib amesema haikuwa lazima kuwaita wadau wa sekta ya habari nchini wakati wa kuandaa rasimu ya muswada wa marekebisho wa sheria ya vyombo vya habari.
Akizungumza katika Ofisi za Bunge jijini Dar es Salaam jana, Waziri Khatib alisema hivi sasa ndio wakati muafaka kwa wadau hao kushirikishwa.
Kauli hiyo inatokana na kuwepo malalamiko kuwa walioshiriki kuandaa muswada huo, hawakutoka taasisi za vyombo vya habari.
Khatib alisema wanasubiri kupata mapendekezo ya muswada huo kutoka kwa wadau hao ambao alisema wameahidi kuyapeleka mwisho mwa mwezi huu, huku akisisitiza kuwa hawana haki ya kukataa muswada.
"Hawana mamlaka ya kukataa, bali kusema tunataka iwe hivi. Wenye mamlaka ya kukataa muswada ni wabunge kwa sababu ndio wawakilishi wa wananchi," alisema.
Kuhusu kubebeshwa lawama na wadau, Waziri Khatib alisema ni halali kwa sababu yeye (Khatib) anamwakilishi Rais katika kuongoza sekta hiyo.
Muswada huo umepata upinzani kutoka kwa wadau, wakidai kuwa unazuia uhuru wa vyombo vya habari na utakuwa kikwazo dhidi ya vita ya kupambana na rushwa na kwamba iwapo utapitishwa utawanyima wananchi kujua masuala yanayofanywa na serikali.
Tayari Baraza la Habari Tanzania (MCT), limeanza kuandaa rasimu mbadala ya muswada huo jinsi wanavyotaka uwe kwa ajili ya kuwasilisha kwa Waziri Khatib.
Chama cha Wamiliki wa Vyombo vya Habari Tanzania (Moat), kimekanusha kuhusika na kukataa muswada huo, na kusema kuwa kilishirikishwa kwenye semina za kujadili muswada huo ambao umekataliwa na asasi nyingi.
Mwenyekiti wa Moat, Reginald Mengi alisema wadau wa sekta ya habari wanaamini watafanikiwa kwenye mapambano ya kusimamisha muswada huo kwa sababu, Rais Jakaya Kikwete ni msikuvu anayepanda uhuru wa kujieleza.