Na Nora Damian
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam jana iligeuka kuwa ulingo wa masumbwi baada ya Mtanzania na raia wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kupigana na kusababisha hakimu kushindwa kuendelea na kesi.
Waliotoa burudani hiyo isiyo na kiingilio ni Lusien Rashidi, raia wa DRC na Mussa Lugandaleta raia wa Tanzania baada ya kubishana kwa dakika kadhaa ndani ya chumba cha mahakama na baadaye kurushiana makonde baada ya Hakimu Mkazi Mkuu, Hamisa Kalombola, kuwaamuru watoke nje.
Katika kesi yao ya madai, inadaiwa kuwa Rashid alimpatia vinyago Lugandaleta vyenye thamani ya Sh 20 milioni ili aviuze kwa makubaliano kuwa kurejesha fedha za mauzo pamoja na faida ndani ya siku 10, lakini hakufanya hivyo.
Rashid aliieleza mahakama kuwa mdaiwa Lugandaleta, alishindwa kulipa fedha hizo na kuanza kumzungusha, huku akitaka kulipa fedha pungufu na walivyokubaliana.
Katika kuutafutia ufumbuzi mvutano huo, Rashid alifungua kesi ya madai katika Mahakama ya Kisutu ili alipwe haki yake.
Jana wakati kesi hiyo ikiendelea, Lugandaleta aliomba mahakama iondoe shauri hilo ili lisuluhishwe nje ya mahakama, lakini mdai alikataa kwa kile alichodai kuwa kibali chake cha kuishi hapa nchini kimeisha hivyo anataka alipwe fedha zake haraka ili aondoke.
“Leo tutalala kitanda kimoja nitakukaba,”alisikika Rashid akimwambia Lugandaleta.
Wakiwa wanalumbana kortini Hakimu aliwaamuru watoke nje na hapo ndipo ngumi zilipoanza baada ya Rashid kumkaba mdaiwa shingoni na kumgandamiza ukutani huku akiita ‘askari, askari njoo’.
Katika kujitetea Lugandaleta alimng’ata kidole gumba cha mkono wa kushoto cha Rashid na kusababisha aanze kupiga kelele, "Wewe unaning’ata unataka kuniambukiza maradhi yako..."
Baada ya sekeseke hilo lilivuta umati wa watu mahakamani hapo, askari waliwaachanisha na kuwachukua na kuwaweka ndani na baadaye kuwapelekwa Kituo cha Polisi cha Kati.
Kesi yao iliahirishwa hadi Februari 23, itakapoendelea kusikilizwa