Na Muhibu Said
MAHUJAJI 277 wakiwamo maofisa watano waandamizi wa Baraza Kuu la Waislamu wa Tanzania (Bakwata) waliomaliza ibada ya hijja nchini Saud Arabia mwishoni mwa mwaka jana wanatarajiwa kuwasili nchini kesho kutwa.
Mahujaji hao wanaoongozwa na Mufti wa Tanzania, Sheikh Mkuu, Issa bin Shaaban Simba, walisafirishwa na Bakwata na taasisi za Taibah na Tanzania Muslim Hajj Trust.
Akizungumza na Mwananchi kwa njia ya simu kutoka Saudi Arabia jana, Katibu wa Kamati ya Umra na Hijja ya Bakwata, Alhaj Imam Swedi Swaibu, alisema mahujaji hao wanatarajiwa kuingia nchini kwa ndege ya Shirika la Ndege la Yemenia saa 10:00 alfajiri kesho kutwa.
Alhaj Swedi, alisema hadi kufikia jana walikuwa bado wako mjini Madina, Saudi Arabia, wakiendelea kutekeleza baadhi ya ibada, ikiwa ni pamoja na kutembelea maeneo mbalimbali matukufu na ya kihistoria ya dini ya Kiislamu yaliyoko mjini humo.
"Tuko ziarani Madina, tunatembelea maeneo ya kihistoria na matukufu na kumaliza siku tisa za swala arubaini," alisema Alhaj Swedi.
Zaidi ya mahujaji 2,000 kutoka Tanzania Bara na Zanzibar, walishiriki ibada ya Hijja, mwaka huu, nchini humo na baadhi yao, walianza kurejea nchini wiki iliyopita. Mahujaji wa Zanzibar, walisafirishwa na taasisi ya Istiqama iliyoko chini ya Idara ya Wakfu na Amana ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ).