Na Ramadhan Semtawa
UZALISHAJI umeme nchini ulioingizwa katika gridi ya taifa umeongezeka kwa kiwango kikubwa hadi kufikia megawati 926 kwa sasa.
Kiwango hicho ni cha juu ikilinganishwa na mahitaji halisi ya juu ya umeme nchini ambayo ni megawati 578.
Wakati umeme uzalishaji ukiongezeka katika kiwango hicho, kiwango cha maji katika bwawa la Mtera nacho kinakariba kufikia katika ujazo wa kawaida kwani hadi sasa bado mita 3.5 juu ya usawa wa bahari.
Ingawa bwawa hilo limebakiza mita za chache za ujazo kufikia katika kiwango chake cha kawaida cha maji ambayo ni mita 696.8 juu ya usawa wa bahari, hadi sasa halijaanza kuzalisha umeme, kwani limewekwa kama akiba ya baadaye.
Katika kipindi cha mwaka jana Tanzania ilikumbwa na ukame uliosababisha upungufu mkubwa wa nishati ya umeme hali iliyosababisha serikali kutafuta umeme wa dharura ambao hadi sasa zimefungwa megawati 62.
Akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi, wakati akifungua mkutano wa wakilishi wa nchi zinazounganishwa na miradi ya bonde la mto Nile (NIB), Naibu Waziri wa Wizara hiyo, William Ngeleja, alisema ongezeko hilo la uzalishaji umeme limekuja wakati tayari Tanzania ilikwishapita katika kipindi kigumu cha ukame.
Karamagi alisema nchi hizo zinapaswa kufahamu changamoto zinazokabili ukanda huo katika suala zima la uzalishaji nishati ya umeme ambazo ni pamoja na ukame.
Waziri Karamagi alisema wataalamu kutoka nchi hizo za bonde la mto Nile wanapaswa kuibua na kuendeleza miradi ya uzalishaji umeme kwa kutumia mbinu mpya zaidi ili iweze kuchangia maendeleo ya kiuchumi ya nchi hizo.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Arthur Mwakapugi, alisema hadi sasa kuna miradi nane tofuati ikiwemo ya uzalishaji umeme inayoendelezwa katika ukanda huo.
Mwakapugi alifafanua kwamba, kwa Tanzania mradi unaendelea kutekelezwa ni wa uzalishaji umeme kwa kuunganisha na nchi jirani ya Rwanda.
Mpango wa maendeleo wa bonde la Mto Nile ulianza mwaka 1999 baada ya mawaziri kutoka nchi kumi ambazo ni Tanzania, Rwanda, Kenya, Uganda, Misri, Ethipia, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC), Uganda, Sudan na Eritrea.
Utekelezaji wa miradi ya NBI ambayo ni pamoja na kilimo, uzalishaji umeme na shughuli nyingine za kiuchumi kutoka nchi fadhiri.