Jeshi la Polisi Nchini, linawashikilia askari sita wa gereza la Kimbiji, Kigamboni, Jijini Dar es Salaam kwa tuhuma za kumuua mfungwa kwa kipigo.
Askari hao wanatuhumiwa kumuua mfungwa aliyekuwa na namba 180/2006 Eradius Stanslaus ambaye alifungwa jela mwaka mmoja katika gereza hilo.
Marehemu na mwenzake mwenye namba A 422/2006, Gome Christopher, walidaiwa kupigwa na askari hao baada ya kutoroka katika gereza hilo Juni 5, mwaka huu.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Waziri wa Mambo ya Ndani, Kapteni (mstaafu), John Chiligati, watuhumiwa hao ni A.9442 Sajini David, A. Koplo Michael, A. 7680 Koplo Rafii, B. 2241 Koplo Abdul, B. 2423 Wdr Heri na B. 3269 Wdr Avith.
Ilisema kuwa, askari hao wamekabidhiwa Jeshi la Polisi ili sheria iweze kuchukua mkondo wake ikiwa ni pamoja na kufikishwa mahakamani kujibu shtaka la mauaji.
Waziri Chiligati alisema katika taarifa yake kuwa, kufuatia kifo cha mfungwa huyo Juni 6, mwaka huu, Kamishna Mkuu wa Magereza aliunda Kamati kuchunguza mazingira ya chanzo cha kifo hicho.
Alisema uchunguzi ulionyesha kuwa, mfungwa huyo na mtoro mwenzake mara waliporejeshwa gerezani, alifungiwa mahali na kupigwa sana na baadhi ya askari wa gereza hilo.