Na Abeid Poyo
MVUTANO kati ya serikali na wadau wa sekta ya habari nchini kuhusu rasimu ya muswada mpya wa sheria ya uhuru wa habari, umechukua sura mpya baada ya wadau wa habari kuamua kuandaa rasimu mbadala ambayo wanapendelea ipelekwe bungeni.
Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari ulioandaliwa na umoja wa taasisi za habari jana katika hoteli ya Peacock jijini Dar es salaam, mwanasheria na Mhadhiri wa Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Dar es salaam Dk Sengondo Mvungi, alisema rasimu hiyo mbadala inatarajiwa kufikishwa serikalini kabla ya mwisho wa mwezi huu.
Aliongeza kuwa rasimu hiyo itakayojumuisha maoni na mawazo ya wadau mbalimbali, italenga kuleta uhuru wa kweli katika upatikanaji wa habari kama inavyoelezwa kwenye ibara ya 18 ya katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Uandaaji wa rasimu mbadala ni pendekezo lililotolewa na wadau wa habari waliokutana Desemba 13 mwaka jana katika Hoteli ya Sea Cliff na kuunda umoja wa taasisi za habari kwa lengo la kuendesha kampeni dhidi ya rasimu ya awali iliyoandaliwa na serikali.
Rasimu ya awali pamoja na megineyo imeelezwa na wadau wa habari kuwa ni ya kikandamizaji inayokiuka haki za msingi za binaadamu.
Umoja huo uliopewa jina la Umoja wa utetezi wa uhuru wa habari na kujieleza, unaundwa na wajumbe kutoka Baraza la Habari Tanzania (MCT), Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (Tamwa) na Taasisi ya Habari ya Kusini mwa Afrika ( MISA-TAN).
Wakati huo huo ripoti ya mapendekezo ya umoja imeshtushwa kuona kuwa rasimu ya serikali imelichukulia suala la habari kama jambo linalowahusu waandishi wa habari tu na hivyo kuweka vipengele vingi vya kuwashughulikia waandishi na taaluma nzima na kutanabahisha kuwa uhuru wa habari ni suala mtambuka linalomhusu kila mtu au kila sekta.
"Ifahamike kuwa haki ya kupata habari ni ya kila raia bila kujali kama ni mkulima, mvuvi, dereva,kuli, waziri ,mbunge, diwani, mwanasiasa," ilisema sehemu ya ripoti hiyo.